SERIKALI imepanga kuanza kupita kila kijiji, mtaa, wilaya, halmashauri na mkoa kusaka vijana wenye vipaji vya sanaa mbalimbali ili kuwasaidia. Anaripoti Kelvin Mwaipungu…(endelea)
Kauli hiyo imetolewa bungeni jijini Dodoma, leo tarehe 2 Februari, 2022 na Waziri wa Utamaduni Sanaa na Michezo, Mohamed Mchengerwa wakati nakijibu swali la Mbunge wa Viti maalumu, Sylivia Sigula (CCM).
Mbunge huyo katika swali lake la nyongeza aliuliza, ni upi mpango wa Serikali kuibua kuendeleza vipaji vya vijana.
Akijibu swali hilo Mchengerwa amesema tayari Rais Samia Suluhu Hassan ameanzisha mfuko maalumu ambao utakwenda kusaidia vijana wenye vipaji.
“Mimi na wasaidizi wangu tumejipanga katika kila mtaa kutafuta vijana wenye vipaji mbalimbali. Tutapita kila kijiji, mtaa, wilaya, halmashauri na mkoa kuhakikisha tunasaka vijana wenye vipaji na kuwasaidia,”amesema.
Akizungumzia kuhusu matamasha yanayoandaliwa na watu binafsi, Mchengerwa amesema wizara haitakuwa na jambo dogo na kuongeza kuwa kila jambo litakuwa na uzito wake.
“Tutashiriki katika kila kitu kinachofanyika kinachohusu sanaa, utamaduni na michezo ambacho wenzetu katika taasisi mbalimbali wamekuwa wakitusaidia serikali,” amesema.
Aidha, Mbunge wa Mikumi, Dennis Londo (CCM) akiuliza swali la nyongeza amehoji, Serikali haioni umefika wakati kutumia vyuo vya Veta kuibua vipaji hivyo?
Akijibu swali hilo, Mchengerwa amesema pamoja na ushauri huo wanategemea kutumia baadhi ya shule kutengeneza akademi za kuibua vipaji.
“Tutatumia shule zaidi ya 56 kwa ajili ya kuendeleza na kukuza vipaji katika maeneo hayo,” amesema.
Katika swali la msingi, Sigula aliuliza: Je, nini mpango wa Serikali wa kutoa ajira rasmi na zisizo rasmi kupitia tasnia ya Sanaa?
Naye Mchengerwa amesema ili kuwavutia wadau hasa vijana kujiajiri katika sekta ya sanaa, mpango wa Serikali ni kuendelea kuboresha mazingira ya kazi za Sanaa kwa kufanya kwa kuhakikisha vifaa na vitendea kazi vya Sanaa vinapatikana kwa bei nafuu kwa kufanya mapitio kwenye kodi za vifaa hivyo.
Pia kupitia upya tozo kwenye Kanuni za BASATA, COSOTA na Bodi ya Filamu Tanzania ili ziwe Rafiki kwa walipaji.
“Kuanzisha mifumo mbalimbali ya kieleketroniki ya usajili, maombi ya vibali na leseni pamoja na mfumo rasmi wa ukusanyaji mirabaha kutoka kwa watumiaji wa kazi za Sanaa,
“Kujenga miundombinu ya Sanaa kama vile Arts Arena, National Art Gallery na One Stop Center, na kuanzisha Mfuko utakaokuwa suluhisho la kimitaji na mafunzo kwa wadau wa Sekta ya Sanaa,” amesema.
Leave a comment