SERIKALI imetenga Sh. 500 Milioni kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba katika Hospitali ya Busega, Simiyu. Anaripoti Jemima Samwel DMC … (endelea).
Serikali kupitia Ofisi ya Tamisemi imetoa maelezo hayo baada ya Simon Lusengekile, Mbunge wa Busega kuhoji ununuzi wa vifaa hivyo leo Alhamisi Tarehe 29 Aprili 2021, katika kipindi cha maswali na majibu bungeni, jijini Dodoma.
Lusengekile amesema, wananchi wa Kata ya Imalamate yenye vijiji vitatu wilayani Busega, wamejenga zahanati na kumaliza maboma manne kwa maana ya zahanati moja kila kijiji.
“Je, serikali ina mpango gani wa kuwasaidia wananchi hao kuezeka maboma hayo ili waweze kupata huduma za afya kwenye zahanati hiyo?” amehoji Lusengekile.
Serikali imeeleza, mwezi Februari 2021, imeipatia Halmashauri ya Wilaya ya Busega Sh. 150 milioni kwa ajili ya kukamilisha maboma ya Zahanati za Ng’wang’wenge, Sanga na Mkula.
Na kwamba, mwaka wa fedha 2021/22 serikali imetenga Sh. 150 milioni kwa ajili ya kukamilisha maboma ya Zahanati za Imalamate, Ijutu na Busami katika Halmashauri ya Wilaya ya Busega, ili kuboresha huduma za afya katika wilaya hiyo.
“Katika mwaka wa fedha 2018/19, serikali iliipatia Halmashauri hiyo Shilingi bilioni 1.8 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri. Aidha, Februari 2021 Serikali imeipatia Halmashauri ya Wilaya ya Busega Shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa wodi 3 katika Hospitali ya Halmashauri, na imetenga Shilingi milioni 500 katika bajeti ya mwaka wa fedha 2020/21 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba katika hospitali hiyo.
“Pia katika mwaka wa fedha 2017/18, Serikali iliipatia Halmashauri ya Wilaya ya Busega Shilingi milioni 250 kwa ajili ya ukarabati wa Kituo cha Afya Nasa na kukiwezesha kuanza kutoa huduma za dharula za upasuaji,” imeeleza serikali.
Na kuwa, itaendelea kujenga na kukarabati miundombinu ya kutolea huduma za fya nchini ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Busega kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.
Leave a comment