SERIKALI ya Tanzania, imesema itaongeza fedha katika Ofisi ya mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), ili kuiwezesha kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi ikiwemo kuhakikisha miradi mikubwa inatekelezwa kulingana na thamani ya fedha inayotumika. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Akizungumza bungeni jijini Dodoma, wakati anawasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Serikali kwa 2022/23, Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Mwigulu Nchemba, amesema ongezeko hilo litasaidia ofisi ya CAG kuwa na watumishi wa kutosha kwa ajili ya kufanya ukaguzi wa miradi hiyo.
“Napendekeza kumwongezea fedha CAG ili apate watumishi wa kutosha kwa kuajiri na kuwahamisha watumishi kutoka idara yoyote ya Serikali na kuwajengea uwezo kwa mafunzo na weledi wa ukaguzi wa thamani ya fedha ili kuweza kukabiliana na tatizo hili,” amesema Dk. Mwigulu.
Katika hatua nyingine, Dk. Mwigulu amesema Serikali itaendelea kuimarisha vitengo vya ukaguzi wa ndani kwa kuvijengea uwezo wa kitaaluma na kuongeza idadi ya watumishi katika fani mbalimbali kama TEHAMA, uhandisi, ukadiriaji majenzi, wakemia na wanasheria.
“Ili kuondokana na dhana ya wakaguzi wa ndani kuwa na taaluma ya fedha pekee. Aidha, Serikali itafanya marekebisho ya Kanuni za Fedha za Umma kwa kuziwezesha Kamati za Ukaguzi kuwa na wajumbe wa nje watatu ikiwemo Mwenyekiti wa Kamati ya Ukaguzi ili kuongeza uhuru na ufanisi wa kamati za ukaguzi kupitia Muswada wa Sheria ya Fedha wa Mwaka 2022,” amesema Dk. Mwigulu.
Leave a comment