SERIKALI kupitia Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), iko katika hatua za mwisho za uwekezaji wa mradi wa kudhibiti usambaaji wa picha na video za ngono mitandaoni, ili kumaliza changamoto ya mmomonyoko wa maadili. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo Ijumaa, tarehe 10 Februari 2023, bungeni jijini Dodoma, na Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye, akimjibu Mbunge wa Kinondoni, Abbas Tarimba, aliyehoji Serikali ina mpango gani wa kudhibiti picha hizo mitandaoni ili kuokoa vijana ambao ndiyo wahanga wakubwa wa athari za suala hilo.
“Katika maendeleo ya TEHAMA moja ya changamoto kubwa tunayopata ni udhibiti wa baadhi ya taarifa ambazo kwa kweli zinamomonyoa utamaduni na maadili ya nchi yetu. Kupitia TCRA tumeongeza uwekezaji mkubwa na sasa tuko hatua za mwisho kuongeza nguvu kudhibiti movement za picha kama hizo kwa kuweka gate ways,” amesema Nape.
Nape amesema “uwekezaji huu ukikamilika na ufungaji mifumo hii ukikamilika hili tutakuwa tumelidhibiti jambo hili kwa kiwango kikubwa.”
Aidha, Nape amesema kwa sasa Serikali ina uwezo wa kufuatilia na kujua wanaosambaza picha na video za ngono, na kuwoanya wanaojihusisha na vitendo hivyo kuacha mara moja kwa kuwa watachukuliwa hatua za kisheria.
Leave a comment