SERIKALI imesema kuwa inaendelea kutekeleza miradi ya maji nchini ikiwa ni pamoja na mijini na vijiji, anaandika Dany Tibason.
Kauli hiyo ilitolewa jana bungeni na Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Mhandisi, Isack Kamwelwe alipokuwa akijibu swali la msingi la mbunge wa Viti Maalum, Leah Komanya (CCM).
Komanya katika swali lake la msingi alitaka kujua serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha miradi ya maji inanufaisha jamii kama ilivyokusudiwa.
“Serikali utumia gharama kubwa katika utafiti wa maji na miundombinu ya maji, lakini baadhi ya miradi inayokabidhiwa kwa Mamlaka za Maji na Jumuiya ya watumia maji (Cowusa) zinasuasua na kutokufaisha jamii kama ilivyo kusudiwa.
“Je serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha miradi ya maji inanufaisha jamii kama ilivyokusudiwa,” alihoji Komanya.
Akijibu maswali hayo Mhandisi Kamwelwe, amesema serikali inaendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya maji mijini na vijiji.
Katika kuhakikisha miradi hiyo inanufaisha jamii kama ilivyokusudiwa, wizara imeandaa na inatekeleza uundaji, Usajili wa vyombo vya watumiaji maji (Cowsos)na kuzijengea uwezo kwa ajili ya uendeshaji na usimamizi.
“Katika kuhakikisha Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira zinatoa huduma mbalimbali endelevu, mamlaka hizo zinasimamiwa na bodi ambazo zinajumuisha wadau mbalimbali” amesema Mhandisi Kamwelwe.
Amesema pamoja na utekelezaji huo lakini kuna changamoto mbalimbali katika miradi hiyo ikiwemo, Uchakavu wa Miundombinu ya Maji, wizi wa vifaa vya maji pamoja na watumiaji wa maji kutolipa huduma hiyo zikiwemo taasisi serikali.
“Hali hiyo ya baadhi ya taasisi za serikali kutolipa madeni yao, kumepelekea mamlaka nyingi kushindwa kugharamia matengenezo ya miundombinu ya maji,” amesema.
Leave a comment