SERIKALI ya Tanzania imesema, itaanzisha mashindano ya uandishi wa Insha kuhusu masuala ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, ili kuwawezesha vijana kufahamu historia ya nchi yao. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Hayo yamesewa leo Jumatatu tarehe 26 Aprili 2021, na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais- Muungano na Mazingira, Selemani Jafo katika Kongamano la Maadhimisho ya Miaka 57 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, jijini Dodoma.
Waziri huyo wa masuala ya muungano, amesema wizara yake imeamua kuanzisha mashindano hayo baada ya kugundua vijana wengi hawana elimu ya muungano.
Jafo amemuagiza Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Mary Maganga asimamie uanzishwaji wa mashindano hayo, yatakayoshirikisha wanafunzi wa Shule ya Msingi na Sekondari nchi nzima.
“Nimegundua elimu ya muungano ni muhimu sana na tulikuwa tunateta na wenzangu katika ofisi yangu. Namuagiza Katibu Mkuu tunaenda kuanza shindano la insha kwa shule za msingi na sekondari, kuandika mada kuhusu muungano,” amesema Jafo.
Jafo amesema “tuwashindanishe watoto wetu wa bara na visiwani, wale watakaoshinda tuwape zawadi hasa wale watatu bora.”
Kiongozi huyo amesema, mashindano hayo yatasaidia kuwaongezea uelewa wanafunzi kuhusu agenda za muungano huo ulioasisiwa na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere na Abeid Amani Karume, tarehe 26 Aprili 1964.
“Ninaimani tukiweka insha maalumu, watajitahidi ku-google (kuperuzi mitandaoni) kutafuta material (taarifa) mbalimbali, itakuwa mwanzo wa kujifunza agenda ya muungano,” amesema Jafo.
Leave a comment