WIZARA ya Elimu, Sayansi na Tekinolojia imeahidi kutumia tafiti zinazofanywa na wanafunzi wazawa ili kugundua matatizo ya wananchi na njia za kuweza kuyatatua, anaandika Angel Willium.
Serikali imetoa kauli hiyo kupitia Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Leonard Akwilapo, wakati wa madhimisho ya miaka 40 ya utafiti walioshirikiana na nchi ya Sweden na wanachuo wa Tanzania, yaliyofanyika jijini Dar es Salaam.
Akwilapo amesema watatumia tafiti zilizofanywa na wanafunzi wa vyuo vikuu nchini waliohitimu ngazi ya uzamili na uzamivu za kilimo, maji, mapango na magonjwa mbalimbali yakiwemo malaria na HIV/AIDS.
Katibu huyo amesema tafiti hizo zilizofanywa na wanafunzi hao zitaisaidia serikali kujua matatizo ya wananchi na njia zipi zitumike kuyatatua.
“Kupitia msaada kutoka Sweden, wanafunzi wamefanikiwa kufanya tafiti hizo, imani yetu watakuwa msaada mkubwa kwa kufumbua matatizo na kukabiliana nayo,” amesema Akwilapo.
Naye Mkurugenzi wa Sayansi za Uhai katika Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia, Bakari Msangi amesema maadhimisho hayo wanaonyesha yale waliofanyia utafiti, wakishirikiana na nchi ya Sweden ambao pia wanafadhili fedha za kufanikisha tafiti hizo.
Kwa upande wake mmoja wa wanachuo waliofanya moja ya tafiti hizo, Dk. Lwidiko Edward, amesema amepata fursa ya kufanya utafiti katika ugonjwa wa malaria hivyo wanafanya uchunguzi wa dawa ya mseto ni namna gani itaweza kutibu ugonjwa na ziendelee kufanya kazi kwa muda mrefu.
Sweden imeanza kuisaidia Tanzania katika tafiti mbalimbali tangu mwaka 1976, leo wamefanya madhimisho ya miaka 40 wakishirikiana na vyuo vikuu nchini kikiwemo Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Leave a comment