SERIKALI imesema iko katika taratibu za mwisho za kuwaajiri walimu 4,500 wa masomo ya sayansi kwa ajili ya kuwapeleka katika shule za sekondari ambazo zina uhaba wa walimu. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Hayo amesema Naibu Waziri Ofisi ya Rais-Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Mwita Waitara leo tarehe 23 Aprili 2019 bungeni jijini Dodoma, wakati akijibu kuhusu mjadala wa uhaba wa walimu wa masomo ya sayansi katika shule za sekondari nchini.
Waitara amesema walimu hao watakapoajiriwa, watapelekwa katika maeneo yenye upungufu wa walimu hasa wa masomo ya hisabati.
Aidha, Waitara amesema baada ya walimu hao kuajiriwa, serikali itaajiri tena walimu kwa awamu ya pili ili kuondoa changamoto ya uhaba wa walimu wa masomo ya Sayansi.
“Ni kweli kuna upungufu, tuna fanya mchakazo zaidi ya walimu 4500 wataajiriwa, wilaya yako ya Kongwa na Buhigwe tutazingatia maeneo yenye upungufu zaidi, na kama kuna maeneo hakuna kabisa walimu, awamu ya pili tutapeleka walimu kadiri ya uwezo utakapopatikana, “ amesema Waitara.
Kufuatia kauli hiyo ya Waitara, Spika wa Bunge, Job Ndugai ameishauri serikali kuajiri walimu wengi wa somo la hisabati akisema kwamba kuna changamoto nyingi ya uhaba wa walimu wa somo hilo.
“Shule nyingine kuna mwalimu mmoja kwa shule nzima, safari hii tupate walimu wa hesabu tu. Hata kama 3,000 au 4,000,” amesema Spika Ndugai.
Leave a comment