SERIKALI imesema kuwa haina takwimu za watoto waliokeketwa nchini kwa kuwa vitendo vya ukeketaji kufanyika kwa siri, anaandika Dany Tibason.
Mbali na kutokuwa na takwimu sahihi za watoto waliokeketwa pia serikali imesema kuwa haina takwimu ya watuhumiwa wa vitendo hivyo ambao mpaka sasa wamepelekwa mahakamani mpaka sasa.
Kauli hiyo imetolewa na bungeni leo na Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Dk Khamisi Kigwangwala alipokuwa akijibu swali la nyongeza la mbunge wa Viti Maalum, Anna Gidarya (Chadema).
Mbunge huyo akiuliza swali la nyongeza, alitaka kujua kama serikali ina takwimu za watoto waliokeketwa pamoja na kutaka kujua kama serikali ina takwimu za watu waliopelekwa mahakamani kutokana na vitendo vya ukeketeaji.
Awali katika swali la msingi la ambunge huyo alitaka kujua serikali ina mpango gani wa kukabiliana na ukatili ambao wanafanyiwa watoto wa kike kwa kukeketwa.
“Mkoa wa Manyara ni mojawapo ya mikoa inayoongoza kwa ukeketaji wa watoto wa kike takwimu za mwaka 2017 zinaonesha kuwa mkoa huo unaongoza kitaifa.
“Je serikali ina mpango mathubuti wa kukomesha ukatili huu wa kijinsia pamoja na kutoa semina elekezi kuhusu madhara yanayotokana na ukeketaji wa watoto wa kike hususani wilaya ya Hanang’, Simanjiro, Kiteto na Mbulu.
“Ngariba sasa wanatumia njia mbadala za kuwakeketa watoto wa kike wa kuanzia miezi sita hadi mwaka mmoja na miezi sita, je serikali ina mkakati gani wa kuwakamata ngariba,wote wanaofanya ukatili huo kwa kuwachukulia hatua ili wawe sehemu ya fundisho ili kukomesha ukatili huo” alihoji Mbunge.
Akijibu maswali hayo Dk. Kigwangwala alisema vitendo vya ukeketaji vinafanywa kwa siri zaidi hivyo serikali haina takwimu za watoto waliokeketwa wala waliopelekwa mahakamani.
Hata hivyo, alisema kuwa serikali inatoa makatazo ya kuwakeketa watoto wa kike kwani kwa kufanya hivyo ni kuwanyanyasa kijinsia watoto wa kike.
Amesema kwa sasa serikali inatoa elimu kwa ngariba wote katika mikoa ambayo bado inaendelea kukeketa watoto wa kike ikiwamo kuwaeleza madhara ukeketaji.
Leave a comment