MJADALA wa Katiba mpya umeendelea kuchukua sura mpya baada ya vyama 11 visivyokuwa na wabunge bungeni kuiomba Serikali ya Tanzania kuufufua mchakato wa katiba kwa kuitisha kura ya maoni ya katiba inayopendekezwa. Anaripoti Victoria Mwakisimba, TUDARCo … (endelea).
Vyama hivyo vya DP, NRA, ADC, AAFP, UDP, SAU, UMD, TLP, CCK, NLD na UPDP vimesema, mabilioni ya fedha yaliyotumika hadi kupatikana kwa Katiba inayopendekezwa “hatuhitaji kupoteza mabilioni mengine, kwa hiyo tusonge mbele kuanzia pale tulipoishia.”
Wametoa kauli hiyo leo Alhamisi tarehe 19 Agosti 2021, mbele ya waandishi wa habari mkoani Dar es Salaam huku wakiwashukia baadhi ya viongozi wa kisiasa na asasi za kiraia.
Mchakati wa katiba ulikwama Aprili 2015 baada ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kutangaza kusitishwa kwa kura ya maoni iliyokuwa ifanyike mwezi huo. Ni baada ya kutokukamilika kwa uandikiaji wa daftari la kudumu la wapiga kura.
Katibu mkuu wa DP, Abdul Mluya akizungumza kwa niaba ya wenzake amesema, “uala la katiba ni suala mtambuka. Uliishia kwenye kura ya maoni na sisi msimamo wetu, tunadhani huu ni muda sahihi wa kwenda kupigia kura ya katiba pendekezwa.”
“Katiba hii pendekezwa ni nzuri, ina maoni yote ya wananchi sasa wale ambao wanataka kuturudisha nyuma wana agenda yao. Twendeni kwenye kura ya maoni na kama kuna madai mengine yataingizwa baadae lakini kwa sasa tuipigie kura kwanza,” amesema Mluya
Katibu mkuu huyo amesema, hata Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan hajatakaa uwepo wa katiba mpya lakini ameomba apewe muda aimarishe uchumi ambao umetikishwa na janga la corona.
“Sina hakika kama Rais amesema hataki katiba mpya bali amesema tumpe muda ajenge nchi, kwa sasa ndio kwanza ana miezi mitano, hata katika ndoa huwezi kuonyesha dira ya familia kwa miezi mitano tu,” amesema Mluya.
Akisisitiza hilo amesema “muda ukifika, badala ya kuturudisha nyuma tuendelee tulipoishia, tusije kutengeneza gharama nyingine kubwa.”
Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa ADC, Doyo Hassan Doyo amesema, baadhi ya viongozi wa vyama vya saisa na asasi za kiraia wana tanguliza mbele maslahi yao binafsi badala ya Taifa na kuwaonya kuacha tabia hizo.
Doyo amesema, kauli za kumlazimisha Rais Samia kufanya yale wanayoyataka wao si jambo zuri huku wakisema wako tayari kukutana na kiongozi huyo mkuu wa nchi ili kujadiliana kuhusu masuala mbalimbali.
Rais Samia amekwisha kuweka wazi kwamba atakutana na viongozi wa vyama vya upinzani ili kujadiliana jinsi ya kuboresha demokrasia.
Leave a comment