SERIKALI ya Tanzania, imewakumbusha wananchi kuzingatia matakwa ya Ibara ya 30 ya Katiba, inayoweka mipaka ya uhuru wa watu. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Wito huo umetolewa leo Jumatano, tarehe 8 Desemba 2021 na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Amon Mpanju, katika mdahalo wa kitaifa juu ya hali ya haki binadamu katika kipindi cha miaka 60.
Ulioandaliwa na Wizara ya Katiba na Sheria, kwa kushirikiana na Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC).
Mpanju amewataka washiriki wa mdahalo huo, kujadili kwa kina matakwa ya Ibara hiyo, kwani haiwezekani kuwa na nchi isiyokuwa na mipaka katika uhuru.
“Naamini mtatueleza maana ya Ibara 30 ya Katiba, ile mipaka inalenga nini. Huwezi kuwa na uhuru usio na mipaka, haiwezi ikawa nchi. Lazima mkubali hapo, maana pana ukakasi lakini huo ni ukweli,” amesema Mpanju.
Mpanju amesema “tunapofanya tathimini tujue masuala ya haki za binadamu yana mipaka yake na ili uzifurahie lazima utimize wajibu.”
Wakati huo huo, Mpanju amesema ili haki za binadamu zikue, inabidi makundi yote yaheshimu mifumo ya katiba na sheria za nchi.
“Lazima uwe na mfumo wa kikatiba, kisheria na wa haki za binadamu unaolenga kukuza haki za binadamu, lakini ndani ya taratibu za kisheria zilizowekwa na hizo sheria ni sharti ziheshimiwe na wadau wote, Serikali, watetezi wa haki za binadamu na wananchi kiujumla,” amesema Mpanju na kuongeza.
“Tumieni uhuru wenu kusema yale mnayoyaona haki kuyasuema, lakini tukiri hauwezi ukaongelea haki bila wajibu, haki yako inapoanzia na inapoishia ndiyo haki ya mwengine inapoanzia, ina maana kuna mipaka katika kufurahia haki zetu na hili wengi huwa hawataki kulisikia.”
Leave a comment