WAZIRI wa Kilimo, Hussein Bashe, amesema wizara yake inafanya maboresho katika sekta ndogo ya mbolea , ili kudhibiti mfumuko wake wa bei nchini. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Bashe amesema hayo leo Ijumaa, tarehe 24 Juni 2022, bungeni jijini Dodoma, akijibu hoja zilizoibuliwa na baadhi ya wabunge kuhusu wizara yake, katika majadala wa makadirio ya mapato na matumizi ya Serikali kwa 2022/23.
“Nataka niwaambie mabadiliko tunayofanya kwenye sekta ndogo ya mbolea, hakuna mtu atakayeweza kutuzuia kwa sababu maboresho tunayofanya ni kwa maslahi ya nchi yetu na maslahi ya wakulima wa nchi hii,” amesema Bashe.
Bashe amesema, ongezeko la bei ya mbolea nchini linasababishwa na kupanda kwa bei ya bidhaa hiyo katika soko la dunia na kwamba, ili kukabiliana na changamoto hiyo, Serikali ya Tanzania imetoa ruzuku kama zinavyofanya nchi nyingine ikiwemo Rwanda, Zambia na Malawi.
Waziri huyo wa kilimo amesema, ruzuku kiasi cha Sh. 100 bilioni zinazotolewa na Serikali kila mwezi, kwa ajili ya kupoza makali ya bei ya mbolea, zitaanza kutolewa kuanzia msimu ujao wa kilimo.
“Tatizo la upandaji wa bei ya mbolea duniani sio tatizo la Tanzania peke yake, Serikali ya Awamu ya Sita imeamua kutoa ruzuku na sisi kama wizara tumejiandaa tunaanza mchakato wa utoaji ruzuku kwenye msimu ujao wa kilimo,” amesema Bashe na kuongeza:
“Na tutavipa kipaumbele viwanda vya ndani, tutavipa ruzuku na wakati huo huo mbolea kutoka nje tutazipa ruzuku.”
Leave a comment