ENDAPO hatua hazitachukuliwa, saratani ya matiti inaweza kushika nafasi ya kwanza, kwa kuwa na idadi kubwa ya wagonjwa nchini. Anaripoti Hamis Mguta … (endelea).
Kauli hiyo imetolewa na Dk. Crispian Kahesa, Mkurugenzi wa Huduma za Kinga ya Saratani katika Taasisi ya Saratani ya Ocean Road (ORCI), leo tarehe 31 Oktoba 2019 mbele ya wanahabari.
Akizungumza kuhusu mwezi wa uhamasishaji, uelimishaji na uchunguzi wa saratani ambao huadhimishwa Oktoba kila mwaka amesema, saratani ya matiti inaongezeka nchini.
“Idadi ya saratani ya matiti, inaonekana kuongezeka nchini ambapo hivi sasa wanawake wenye umri kuanzia miaka 20 na kuendelea, nao wanagundulika kuugua ugonjwa huu.
“Hatua zisipochukuliwa, saratani hiyo itazidi kuwa tishio zaidi. Idadi kubwa ya wagonjwa wanaofika hospitalini hapa wanatoka katika maeneo ya mijini,” amesema.
Inaelezwa, miaka iliyopita wagonjwa wa saratani ya matiti walikuwa ni kuanzia miaka 55, lakini ikashuka hadi miaka 50 na sasa wenye umri wa miaka 20.
Kwa upande wa wanaume, Dk. Kahesa amesema saratani hiyo huathiri asilimia moja kwa wanaume, hata hivyo kwa upande huo ni hatari zaidi na kwamba endapo isipogundulika haraka, huweza kuathiri mapafu kwa haraka.
“Saratani hii huathiri wanawake zaidi kuliko wanaume kwa asilimia 99, na wanaume ni asilimia 1 tu. Dalili kwa wanaume ni tofauti kidogo na wanawake, hivyo kwa mwanaume ni rahisi kugundua kuliko mwanamke kwa kuwa kifua chake kina mafuta mengi,’ amesema.
Ameongeza, kati ya wanawake 170 waliofanyiwa vipimo, zaidi ya 68 waligundulika na uvimbe ambao ni ugonjwa wa saratani.
Leave a comment