SARAH Obama (99), Bibi wa Rais wa zamani wa Marekani, Barrack Obama, amefariki dunia leo Jumatatu tarehe 29 Machi 2021, katika Hospitali ya Jaramogi Oginga Odinga, Kisumu, nchini Kenya alipokuwa akipatiwa matibabu. Anaripoti mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Marsat Obama, mtoto wa Sara akizungumza na mtandao wa Daily Nation la Kenya amesema, mama yake amefariki alfajili ya saa 4:45, baada ya kufikishwa hospitalini hapo jana Jumapili kwa ajili ya matibabu.
Amesema, mama yake (Sarah), alikuwa mgonjwa wa kiharusi alichokipata kuanzia Septemba 2020 pamoja na kisukari.
Marsat amesema, mpango wa mazishi yanaendelea ambapo yanatarajiwa kufanyika leo Jumatatu au kesho katika makaburi ya Kiislamu yaliyopo Kisumu.
Kutokana na kifo hicho, Uhuru Kenyatta, Rais wa Kenya ametuma salamu za rambirambi kwa familia ya Obama akimwelezea Sarah alikuwa nembo ya familia na Kenya itaukumbuka mchango wake.
“Kifo cha Sarah ni pigo kwa taifa letu. Tumempoteza mtu muhimu, tunaungana na familia katika kipindi hiki kigumu wanachokipitia,” amesema Rais Kenyatta
Amesema, Sarah atakumbukwa kwa mchango wake hususan eneo la Nyang’oma Kagelo alipokuwa akifanya shughuli mbalimbali za kimaendeleo.
Leave a comment