MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Samia Suluhu Hassan, ameuagiza Umoja Wanawake ya chama hicho (UWT), umpatie ripoti inayoonesha maendeleo ya mwanamke wa Kitanzania, katika kipindi cha miaka 60 ya uhuru wa Tanganyika. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Samia ambye pia ni Rais wa kwanza mwanamke wa Tanzania, ametoa agizo hilo leo Jumamosi, tarehe 23 Oktoba 2021 katika maadhimisho ya kilele cha wiki ya UWT, yaliyofanyika wilayani Rufiji, Mkoa wa Pwani.
Rais Samia amesema katika maandalizi ya kuelekea maadhimisho ya miaka 60 ya Uhuru wa Tanganyika, UWT iwasilishe taarifa kuhusu safari ya ukombozi wa mwanamke kiuchumi, kisiasa na kifikra, kaunzia 1961 hadi 2021.
“Nilikuwa nanong’oneza na mwenyekiti (Mwenyekiiti wa UWT, Gaudensia Kabaka), hapa. Nilikuwa namuuliza baada ya wiki hii mtakuwa na shughuli nyingine kabla ya miaka 60 ya uhuru? Akaniambia kutakuwa na mkutano mwingine mkubwa,”
“Katika mkutano huo nataka UWT mje na yafuatayo, hali ya kiuchumi ya mwanamke wa Kitanzania baada ya miaka 60 ya uhuru, kutoka tulipoanza 1961, safari yetu katikati hadi leo tulipofika mwanamke wa Kitanzania amesimamaje kiuchumi,” amesema Rais Samia.
Aidha, Rais Samia ameuagiza umoja huo, umpe ripoti juu ya ushiriki wa mwanamke wa Kitanzania katika siasa, tangu enzi za muasisi wa UWT, Bibi Titi Mohammed hadi kipindi hiki ambacho Tanzania ina Rais mwanamke.
“Lakini nataka mje na hili katika nyanja mbalimbali, sio tu katika nyanja ya kisiasa lakini maeneo mbalimbali, lakini pia mje na taarifa inayosema kifikra mwanamke wa Tanzania amekombolewa vipi kutoka enzi za Bibi Titi hadi leo,” amesema Rais Samia.
Aidha, Rais Samia ameiachia kibarua jumuiya hiyo, ijitafakari katika kipindi hicho imetimiza kwa kiasi gani madhumuni ya kuasisiwa kwake, ikiwemo kumkomboa mwanamke wa Kitanzania.
Leave a comment