RAIS Samia Suluhu Hassan ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM ameutaka Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) kuacha kusimama na mtu badala yake isimame na serikali ili kufanya maendeleo ya Taifa bila kujali itikadi za kisiasa
Pia ameutaka umoja huo kujipanga vizuri na kuibua miradi mikubwa kiuchumi ili kuwa na nguvu imara ya kisiasa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Rais Samia ametoa kauli hiyo leo tarehe 28 Novemba, 2022 wakati akifungua Mkutano Mkuu wa 10 wa UWT Taifa – Dodoma ambao umeenda sambamba na kuchagua viongozi wa umoja huo.
Mkutano huo ulikuwa na kauli mbiua inayosema, UWT simama na Samia kwa maendeleo ya Taifa.”
“Nimeona kaulimbiu ya uchaguzi wetu mwaka huu inayosema ‘UWT simama na Samia kwa maendeleo ya Taifa,’ ningependa nifanye marekebisho kidogo, ‘UWT simama na Serikali kwa maendeleo ya Taifa.
“Kwa sababu tukisimama na serikali… tunasimama na taasisi, tukisimama na Samia, tunasimama na mtu. Wenzetu wanatuambia tuwe wa malengo kuliko kusimama na watu na Katibu Mkuu(Daniel Chongolo) amesema,” amesema Rais Samia.
Aidha, ameeleza kusikitishwa na uchache wa idadi ya wanachama wapya 86,288 waliojiunga na UWT kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita kuanzia 2017- 2022.
“Ukichukua idadi hiyo ukiigawa kwa mikoa 32 ambayo ndani yake kuna mikoa midogo kama ya Zanzibar, ina maana kila mkoa umeingiza wanachama wapya 2,697, sasa hii si kazi nzuri kwa sababu tulikuwa na fursa nzuri hasa ikizingatiwa nchi imetulia.
“Hekaheka za kisiasa ambazo zilikuwa zinatushughulisha hazipo, tungetumia muda huu kuweka wanachama wengi zaidi ndani ya UWT kuliko tulivyofanya,” amesema.
Pia ameitaka UWT kutekeleza miradi itakayoupa nguvu umoja huo na kuacha kushikashika hapa na pale.
“Kamati ya maandalizi ya mkutano huu ilihangaika kutafuta fedha huku kule. Hii inaonesha miradi tuliyonayo si miradi mikubwa ya kutupatia nguvu ya kiuchumi katika jumuiya.
“Kama mnavyojua uwezo wa kiuchumi hununua uwezo wa siasa tusiposimama vizuri na kwa sababu hatuna nguvu ya kiuchumi huenda tukanunuliwa kisiasa, naomba tuende tukajipange vizuri na miradi ambayo inaweza ikatupatia nguvu,” amesema.
Aidha, ameitaka UWT kujitathmini katika makongamano inayoshiriki kuisemea serikali.
Pia ameitaka UWT kushirikiana na jamii kikamilifu kupinga vitendo vya udhalilishaji kwa watoto.
Amesema kwa kuwa moja ya majukumu ya UWT ilikuwa ni kujikomboa, tayari Watanzania wameshajikomboa hivyo sasa watanue mbawa zao na kudhubutu kusema na kukemea mambo ambayo yanakwenda kinyume cha taratibu.
“Fanyeni mambo ambayo yatajenga jumuiya yetu kwa sababu chama ni jumuiya zake.Tokeni, shirikianeni fursa ambazo zinaweza kukuza jumuiya zetu kiuchumi. Tuwe wadhubutu, semeni, tuendeni, tusipokuwa wadhubutu hatutakwenda,” amesema.
Leave a comment