RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amekutana na kufanya mazungumzo na Rais Mstaafu wa Nigeria, Olusegun Obasanjo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Mazungumzo hayo, yamefanyika leo Jumatatu, tarehe 3 Mei 2021, Ikulu Chamwino, mkoani Dodoma.
Obasanjo ametoa salamu zake za rambirambi kwa Rais Samia, kufuatia vifo vya waliokuwa marais wa wa Tanzania, Hayati Benjamin William Mkapa na Hayati John Pombe Magufuli.
Hayati Mkapa, alifariki dunia tarehe 23 Julai, 2020 na Hayati Magufuli, aliaga dunia tarehe 17 Machi, 2021.
Rais huyo mstaafu, amempongeza, Rais Samia kwa kupokea kijiti cha kuwa Rais wa Tanzania na amemtakia heri katika majukumu yake.
Aidha, katika mazungumzo hayo, viongozi hao wamezungumzia hali ya usalama Barani Afrika na umuhimu wa wakuu wa nchi kujadiliana na kutafuta suluhisho la migogoro hiyo ambayo inasababisha vifo vya watu wasio na hatia hasa wanawake na watoto.
Pia, viongozi hao, wamezungumzia masuala ya maendeleo hasa katika uchumi na kusisitiza umuhimu wa nchi za Afrika kuongeza ushirikiano na kuondoa vikwazo vya biashara na uwekezaji.
Leave a comment