RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amesema hivi sasa wataachana kwanza na ujenzi wa vituo vipya vya afya na nguvu kubwa itaelekezwa katika kuimarisha huduma katika zahanati na vituo vilivyopo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Rais Samia ameyasema hayo leo Ijumaa Tarehe 30 Septemba, 2022, katika hafla ya utiliaji saini mkataba wa usimamizi wa shughuli za lishe ambayo imenda sambamba na makabidhiano ya vifaa tiba na vitendea kazi katika sekta ya lishe.
“Nilikuwa nanong’ona na Waziri wa afya nikamwambia embu tupige stop kujenga vituo vya afya hususan vya kata tujielekeze zaidi kwenye kumalizia zahanati na kuimarisha huduma kwenye vituo vya kata,” amesema Raais Samia.
Amesema katika kukuza huduma ni kuhakikisha vifaa tiba, wahudumu wa afya wanakuwepo katika maeneo hayo sambamba na nyumba za watumishi.
“Nahisi haya yatasaidia kutoa huduma bora zaidi kuliko kuendelea kujenga, kujenga. Tuimarishe tumalize, tukisimama vizuri huko mbele tutaendelea kuweka vituo maeneo ambayo hayana vituo lakini hivi sasa la muhimu ni zahanati na zahanati zilizotimia lakini kuimarisa huduma katika vituo vya afya na makofi haya yanamaanisha tumekubaliana,” amesema.
Amesema katika kuimarisha huduma za afya maeneo hayo tayari alishamwagiza Waziri wa Tamisemi kutenga Sh 917 bilioni kwaajili ya kupeleka pikipiki kwaajili ya maofisa afya kata.
Alisema pikipiki hizo zitawapa urahisi wa kuzunguka na kufanya ufuataliaji kwenye maeneo yao.
“Hilo halijafanyika lakini tutakuja hapa kufanya makabidhiano ya pikipiki kwaajili ya maafisa afya 917…wapo wengi zaidi ya 2000 nadhani lakini hii ni lot ya kwanza na tutakuwa tunanunua kadiri bajeti itakavyoruhusu na kusambaza mpaka wote wapate hizi pikipiki,” amesema.
Tuna shukuru kwa kuliona hilo.