RAIS Samia Suluhu Hassan ameielekeza Wizara ya Ujenzi kufanya usanifu wa kina wa barabara za Mwanza Mjini hadi Round about ya Usagara na barabara ya Mwanza Mjini hadi Igoma ili zipewe kipaumbele katika bajeti ya mwaka wa fedha 2024/25 kwa ajili ya kujenga barabara ya njia nne. Anaripoti Danson Kaijage, Mwanza (endelea).
Hayo yameelezwa leo Jumapili mkoani Mwanza na Katibu wa Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Paul Makonda alipotembelea ujenzi wa Daraja la JP Magufuli (Kigongo- Busisi) ambalo ujenzi wake umefikia asilimia 80.
“Rais, Dk. Samia Suluhu Hassan amenielekeza ufanyike haraka sana usanifu wa kina wa barabara mbili, barabara ya Mwanza Mjini Kwenda Usagara Kilometa 22 na Mwanza Mjini kuelekea Igoma ili ziwekwe kwenye vipaumbele vya bajeti ya 2024/25 kujengwa kwa njia nne” amesem Makonda.
Makonda amesema daraja la John Magufuli ni la kimkakati kwani mkoa wa Mwanza upo katikati ya nchi za Afrika Mashariki, hivyo itakuwa ni njia ya mkato wa kufikia nchi jirani.
“Wananchi kutoka DRC, Uganda, Rwanda, Burundi wote watatumia daraja hili kufikisha bidhaa kwenye nchi zao pia kupitia ujenzi wa Reli ya Kisasa ya SGR daraja hili litatumika kupitisha malori yenye mizigo mikubwa kufika huko”, amesema Makonda.
Aidha, Bashungwa amesema Rais tayari ametoa kibali kwa mwaka huu wa fedha kujenga barabara ya kutoka Airport- Igombe hadi Nyanguge yenye urefu wa kilomita 46 iliyopo kwenye bajeti ya mwaka wa fedha 2023/24 kwa kuanza kujenga kwa kiwango cha lami kilomita 10.
Bashungwa ameongeza kuwa kwa kutambua umuhimu wa Daraja la JP Magufuli katika kuunganisha ushoroba wa Ziwa Viktoria unaoanzia Sirari mpakani mwa nchi ya Tanzania na Kenya hadi Mutukula Mpakani mwa Tanzania na Uganda, barabara hiyo itapanuliwa na kuwa na njia nne ili kupunguza msongamano wa magari.
“Mwelekeo huu ni sambamba na kukamilika kwa daraja la JPM, Ujenzi wa SGR, Vivuko vinne vipya na vitano vinavyokarabatiwa, haya yote yanaenda kulifanya jiji la Mwanza kuwa moja ya majiji bora ukanda huu wa Afrika” amesisitiza Bashungwa.
Naye Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Amos Makala, amesema ujenzi wa daraja hilo una manufaa makubwa na likikamilika utaokoa muda wa wananchi kusubiri vivuko kwani sasa watatumia dakika tatu hadi nne kuvuka kwenda upande wa pili wa Busisi.
Leave a comment