WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Masauni, amempa siku saba Inspekta Jenerali wa Polisi nchini (IGP), Simon Sirro, adhibiti matukio ya uhalifu yanayofanywa na kundi la vijana linalotumia silaha za jadi kujeruhi wananchi na kupora mali zao maarufu kama Panya Road. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Mhandisi Masauni ametoa maagizo hayo mbele ya IGP Sirro, jana Jumanne, tarehe 3 Mei 2022, alipotembelea wananchi wa Chanika, jijini Dar es Salaam, waliojeruhiwa na kuporwa mali zao na Panya Road, hivi karibuni.
“Hatutegemei baada ya siku saba tuone raia wowote wa Dar es Salaam amekatwa panga,” amesema Mhandisi Masauni.
Aidha, Mhandisi Masauni amelitaka Jeshi la Polisi, kuwachukulia hatua za kisheria wananchi wanaolinda na kuwaficha wahalifu, ikiwemo Panya Road.
“Hawa wazee wanaolinda wezi, kwani anayelinda mwizi naye si mwizi? Kwani anayelinda mhalifu naye si mhalifu? Kwa nini msianze na hao?” amesema Mhandisi Masauni.
Awali, katika mkutano huo baadhi ya wananchi walifikisha malalamiko yao kwa Mhandisi Masauni, wakidai wanatoa taarifa za wahalifu kwa Maafisa wa Polisi, lakini hazifanyiwi kazi, ambapo Waziri huyo wa Mambo ya Ndani ya Nchi, aliwataka wawaripoti Polisi wanakiuka maadili yao ya kazi.
“Kuna mama anazungumza watu wanatoa taarifa lakini hazifanyiwi kazi, mimi ni imani yangu kwamba, kama kuna watu wanafanya hivyo watakuwa ni wachache. Wenyewe wanatakiwa zitolewe taarifa dhidi yao, kuna utaratibu wa kutoa taarifa dhidi ya askari wanaokiuka maadili yao,” amesema Mhandisi Masauni.
Kufuatia maagizo hayo, IGP Sirro alimuomba radhi Mhandisi Masauni kufuatia changamoto hiyo, huku akimuahidi atajirekebisha kwa kutokomeza vitendo vya kihalifu.
“Ningependa niyasikie haya maneno Burundi na Rwanda, lakini mahali anapoishi IGP Sirro (Chanika), unafanya haya ni kunidhalilisha na kunidhalilisha maana yake kesho Waziri utanipiga chini , halafu itakuwa balaa na muda wangu umekaribia, naomba mnihurumie nitajirekebisha,” amesema IGP Sirro.
Leave a comment