NAPE Nnauye, Mbunge wa Mtama amewataka watu wanaojadili sauti iliyosambaa mitandaoni inayodaiwa kuwa ni yake na Abdulrahman Kinana, Katibu Mkuu Mstaafu wa CCM, waweke akiba ya maneno. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Nape ametoa kauli hiyo jana tarehe 19 Julai 2019, kuhusu tuhuma za kuisaliti CCM, zilizoibuka baada ya sauti inayodaiwa kuwa ni ya mazungumzo yake na Kinana wakijadili muenendo wa chama chao, kuvuja.
Akizungumzia sakata hilo, Nape amesema suala hilo siyo la kawaida kwani limebeba jinai, hivyo wanaolijadili wawe na mipaka, ili wasije kuwa sehemu ya jinai.
“Suala hili sio la kawaida kabisa lakini huwa inatokea, nachotaka kusema ni kwamba wanaojadili waendelee kujadili pengine wachukue tahadhari waweke akiba ya maneno. Wasije wakawa sehemu ya jinai yenyewe.
Sababu mnaweza kuajdili, lakini kuna sheria zinaendesha haya mambo ndio maana mimi mwenyewe naweka mipaka ya kujadili. Ukilijadili sana mkafikisha mahali na nyie mnaojadili mkashiriki jinai,” amesema Nape.
Nape ameeleza kuwa, suala hilo ni vyema likaachwa kwa mamlaka husika, ili zifanye kazi yake kwa mujibu wa sheria.
“Kwa hili sauti kusambaa nadhani ni vizuri tukaviachia vyombo vinavyohusika, ambavyo kazi yake ni kushughulikia mambo hayo. Bila shaka watashughulikia na watakapoona undani wake, wataona kama iko haja ya kuchukua hatua kwa mujibu wa sheria sababu sheria zipo zinazozungumzia suala hili,” ameshauri Nape.
Hivi karibuni katika mitandao ya kijamii ilisambaa sauti inayodaiwa kuwa ni mazungumzo ya Nape na Kinana, ambapo maudhui yake yalilenga kuukosoa uongozi wa CCM na serikali.
Sauti hiyo ilivuja baada ya Mzee Makamba na Kinana mnamo tarehe 14 Julai mwaka huu, kutoa waraka wakihoji ukimya wa serikali kuhusu tabia ya Mwanaharakati, Cyprian Musiba kutoa tuhuma nzito dhidi ya baadhi ya viongozi wastaafu wa serikali na CCM pamoja na wanasiasa, ya kwamba wanamhujumu Rais John Magufuli.
Leave a comment