SAKATA la mlinda mlango wa Yanga na timu ya Taifa ya Tanzania, Metecha Mnata limechukua sura mpya baada ya uongozi wa klabu hiyo na meneja wa nyota huyo kuzungunza juu ya sintofahamu kuhusu taarifa aliyoiweka kwenye mitandao ya kijamii. Anaripoti kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Jana kupitia ukurasa wake kwenye mtandao wa kijamii wa Instagram majira ya saa 2 usiku, mlinda mlango huyo aliandika taarifa iliyotafsilika kama anaondoka klabuni hapo mara baada ya kuhudumu kwa muda wa miaka miwili.
“Nawashukuru kwa wote na pia kwa kunipa sapoti katika miaka miwili na nilifurahi maisha yangu nikiwa Yanga kila la heri katika mafanikio yenu.”
Baada ya taarifa hiyo katibu mkuu wa Yanga Haji Mfikilwa alisema kuwa, taarifa hiyo wameona kupitia mitandaoni kama walivyoona wengine lakini yeye mwenyewe anajua anamaamisha nini lakini bado yeye ni mchezaji wa Yanga.
“Na sisi tuliziona kama wewe ulivyoziona kwenye mitandao, hatujapata kuzungumza nae kuhusu jambo hilo, yeye mwenyewe ndio anajua Zaidi alikuwa anamaanisha nini.
“Kila mchezaji anafikra zake na maamuzi yake jambo hilo limetokea usiku na sisi tumeamka asubuhi, jana tulimtafuta hakupatikana na niwaambie tu watu wasiwe na taharuki, tutaliweka sasa,” alisema katibu huyo.
Meneja wa mchezaji huyo, Jemedari Said alisema kuwa Metacha bado ni mchezaji wa Yanga na amezungumza nae jana na kumueleza kuwa amekosea licha ya kupata msukumo kutoka kwa kiongozi.
“Metacha mchezaji wa Yanga, ni kawaida inapotokea baadhi ya vitu kusumbua kidogo, Metacha amepata presha tena amepata msukumo kutoka kwa kiongozi, huo msukumo ungetoka nje isingekuwa shida.
“Nimeongea naye jana nimemwambia ulichofanya umekosea, yeye bado kijana mdogo hajakaa kwenye timu kubwa zenye presha kama hivi, nikubali kuwa amefanya kosa lakini na yeye amekosewa,” alisema Meneja huyo.
Kwa sasa Metacha amejiunga kwenye kambi ya timu ya Taifa ya Tanzania ambayo inajiandaa na michezo miwili ya kirafiki pamoja na mchezo mmoja wa kufuzu kwa michuano ya AFCON dhidi ya Equatorial Guinea.
Klabu ya Yanga kwa siku za hivi karibuni imekuwa kwenye presha kubwa kufuatia matokeo mabaya waliyopata kwenye michezo sita ya Ligi Kuu mpaka kupelekea kuvunja benchi lote na ufundi.
Leave a comment