MAHAKAMA Kuu ya Zanzibar imewaamuru Kamishna wa Polisi Zanzibar na Naibu Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai Zanzibar (DCI), kufika mahakamani kwa ajili ya kujieleza kwa nini hawajatoa dhamana au kuwafikisha mahakamani wanachama wa ACT-Wazalendo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar … (endelea).
Wanachama hao wakiongozwa na Naibu Katibu Mkuu wa ACT-Wazalendo, Ahmed Nassor Mazrui wanashikiliwa na polisi kwa zaidi ya siku 12 tangu walipokamatwa kwa nyakati tofauti wakati wa maandamano ya amani kupinga matokeo ya Uchaguzi Mkuu uliofanyika tarehe 27 na 28 Oktoba 2020.
Mahakama hiyo imetoa amri hiyo leo Alhamisi tarehe 12 Novemba 2020, wakati inasikiliza shauri lililofunguliwa na ACT-Wazalendo dhidi ya DCI na Kamishna Mkuu wa Polisi visiwani humo, kikiitaka mahakama hiyo itoe amri ya watuhumiwa hao kufikishwa mahakamani au kuachiwa huru.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mwanasheria Mkuu wa ACT-Wazalendo, Omar Said Shaabani, vigogo hao wametakiwa kufika mahakamani hapo kesho Ijumaa tarehe 13 Novemba 2020 kwa ajili ya kujieleza.
Shaabani amesema, amri hiyo ya Mahakama Kuu ya Zanzibar imetolewa baada ya mahakama hiyo kusikiliza upande mmoja wa shauri hilo.
“Leo 12 Novemba 2020, ombi letu la Habeas Corpus kuiomba mahakama itoe amri Mazrui na wenzake waachiwe au waletwe Mahakamani, limesikilizwa upande mmoja na Mahakama imetoa amri ya kumuita Kamishna wa Polisi Zanzibar na DCI wafike mbele ya mahakama kesho tarehe 13 November, 2020 asubuhi kwa ajili ya kujieleza,” inaeleza taarifa ya Shaabani.
Maandamano hayo yaliyofanyika tarehe 2 Novemba 2020 yaliitishwa na ACT-Wazalendo na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).
Vyama hivyo vimepinga matokeo hayo yaliyotangazwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi Tanzania (NEC) na Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) kwa madai kulikuwa na ukiukwaji mkubwa wa sheria na kanuni za uchaguzi.
Matokeo hayo yanayopingwa na vyama hivyo, yalikipa ushindi wa kishindo Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika nafasi za Urais wa Tanzania na Zanzibar, ubunge, uwakilishi na udiwani.
Leave a comment