JESHI la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, limekemea tabia ya wasanii kuvunja sharia hasa kusambaza picha za utupu. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Onyo hilo limetolewa leo Jumanne tarehe 20 Aprili 2021, na Kamanda wa Polisi wa kanda hiyo, SACP Lazaro Mambosasa, akizungumza na wanahabari kuhusu sakata la kusambazwa kwa picha za utupu za msanii, Rajab Kahale ‘Harmonize’, jijini Dar es Salaam.
“Niwaonye wasanii, tuna waheshimu sana ni kada nzuri, waheshimiane lakini kila wanachofanya wajaribu kujiuliza kabla ya kufanya, kwa kufanya hivi sijavunja sheria za nchi?
“Ukikuta unavunja sheria ya nchi, aghirisha kabla hujatenda, vinginevyo hatutaangalia mtu kwa heshima yake au kwa nafasi yake, akitenda kosa atashughulikiwa kama waharifu wengine,” amesema Kamanda Mambosasa.
Kamanda Mambosasa amesema, wasanii wanaongoza kusambaza picha za utupu kwa ajili ya kuwashushia heshima wengine katika jamii.
“Wasanii wamekuwa watumiaji wabaya wa mitandao, kwa maana ya kurushiana picha. Unajua wanahasimiana kundi na kundi, kwa ajili ya kushushiana hadhi, usanii ni biashara lakini biashara yenye competition (ushindani) kubwa,” amesema Kamanda Mambosasa na kuongeza:
“Watu wanaotaka kufanana kiviwango hata siku moja hawapendani, wanakuwa mmoja anataka amzulie mwenzake hili, mwingine amzulie hili. Wakijaribu kumshusha wakati anatafuta yeye kupanda.”
Akizungumzia sakata la Harmonize, Mambosasa amesema hadi sasa wamewahoji watu watano, wanao tuhumiwa kuhusika katika sakata hilo.

Watu hao ni msanii wa Bongo Movie Frida Kajala Masanja (36) na mwanaye Paula Paul Peter (18). Wasanii wa Bongo Fleva ni Raymond Shabani Mwakyusa ‘Ray Vann’ (27), Claiton Revocatus ‘Baba Levo’ (34), Catherine John Charles na Juma Haji (32).
“Jeshi la Polisi la Polisi kanda maalum ya Dar es salaam linaendelea kuchunguza tuhuma za kusambaa picha za utupu za msanii wa muziki wa kizazi kipya anayefahamika kwa jina la Harmonize.
“Hadi sasa wamehojiwa watuhumiwa watano,”amesema Kamanda Mambosasa na kwamba watuhumiwa hao wameachiwa kwa dhamana.
Kamanda Mambosasa amesema upelelezi wa tuhuma hizo unaendelea kufanyika kwa ajili ya kufikisha jalada kwa mwanasheria wa kanda hiyo, kwa taratibu nyingine za kisheria.
Leave a comment