HELLEN Kijo-Bisimba, Mkurugenzi Mtendaji Mstaafu wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu Tanzania (LHRC), amewashauri wadau wa Tasnia ya Sheria kupaza sauti zao juu ya tukio la Fatma Karume kuondolewa katika orodha ya mawakili wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS). Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Kijo-Bisimba amesema hayo leo Ijumaa tarehe 25 Septemba 2020 katika hafla ya maadhimisho ya miaka 25 ya LHRC iliyofanyika ukumbi wa mikutano wa Kimataifa Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam.
Tarehe 23 Septemba 2020 Kamati ya Maadili ya Mawakili ilimuondoa Fatma katika orodha ya mawakili kwa upande wa bara, baada ya kumkuta na hatia katika tuhuma za kuishambulia Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, zilizoibuka Septemba 2019.
Akizungumzia sakata hilo, Kijo-Bisimba amesema uamuzi wa Fatma Karume kuvuliwa uwakili umeacha maswali mengi na kuwaomba wanasheria kupaza sauti zao ili kupata ufafanuzi wa maswali hayo.

“Uogo hauna maana, hofu haina maana kusema kunasaidia kubadili watu lakini watu wakipata hofu si jambo jema. Watu wanaogopa kusema suala la mwanaharakati Fatma Karume amevuliwa vyeo upande wa kulia lakini kuna maswali lazima tuulize kama wanasheria tusinyamaze,” amesema Kijo-Bisimba.
Sakata la Fatma kuvuliwa uwakili kwa upande wa Tanzania Bara limekuja siku kadhaa baada ya mwanaharakati huyo kuondolewa katika Kampuni ya Wanasheria ya IMMMA, ambayo alikuwa sehemu ya mwanzilishi wake.
Fatma ambaye ni mtoto wa Rais mstaafu wa Zanzibar, Aman Abeid Karume aliondolewa katika kampuni hiyo tarehe 16 Septemba 2020 baada ya washirika wenzake katika IMMMA Advocates kuvunja mkataba wa ushirikiano naye.
Leave a comment