NGOME ya Vijana ya Chama cha ACT-Wazalendo, imetangaza nia yake ya kufanya maandamano ya amani kupinga azimio la Bunge kuacha kufanya kazi na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali Tanzania (CAG), Profesa Mussa Assad. Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo tarehe 6 Aprili 2019 na Katibu wa Ngome ya Vijana ya ACT-Wazalendo, Isack Nyasilu.
Imeeleza kwamba, inapinga vikali azimio hilo ikidai kwamba, likitekelezwa litakuwa na athari kubwa kwenye mfumo mzima wa uwajibikaji na uwazi.
“Tuna imani kuwa, hatua hii ya bunge inalenga kuzuia ripoti ya CAG kusomwa bungeni,” inaeleza sehemu ya taarifa ya Nyasilu.
Kwa mujibu wa taarifa ya Nyasilu, ngome hiyo imetuma barua ya mualiko wa kushiriki maandamano hayo kwa viongozi wa vijana wa vyama vya upinzani nchini, kwa ajili ya kushirikiana kuandaa maandamano ya kupinga azimio hilo la Bunge.
“Ngome ya Vijana inapinga vikali azimio hili kwa nguvu zote kwa sababu linaenda kuua msingi wa uwazi na uwajibikaji, Ngome inapingana na utetezi wa Spika Job Ndugai kuwa, imesitisha kufanya kazi na CAG na sio ofisi ya CAG.
“Jambo hili ni la kuduwaza sana kwa sababu Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania haizungumzi kuhusu Ofisi ya CAG bali inamtaja CAG mwenyewe kwa jina,” ianeleza taarifa hiyo.
Leave a comment