HATUA ya Roeland van de Geer, aliyekuwa Balozi wa Umoja wa Ulaya (EU) nchini Tanzania kuondoka na kurejea kwao kwa shinikizo, sasa imehojiwa bungeni. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni leo tarehe 30 Mei 2019, imeitaka maelezo ya serikali sababu za balozi huyo wa EU, kuwekewa shinikizo na hata kuondoka nchini bila kutoa taarifa yoyote rasmi.
Salome Makamba akisoma taarifa ya Kambi Rasmi ya Upinzani kwa niaba ya Waziri Kivuli wa Wizara ya Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Esther Matiko amesema, EU ni miongoni mwa wadau wakubwa wa maendeleo nchini na kwamba, kuondoka kwake kuna athari kubwa si kwa CCM bali kwa Watanzania.
Taarifa za kuondoka ghafla Roeland zilisambaa mwanzoni mwa Novemba 2018 ambapo zilieleza kuwa, balozi huyo alifukuzwa nchini. Hata hivyo, serikali ilitoa taarifa kwamba, hakufukuzwa bali aliitwa kwao Ubelgij ili kushauriana kuhusu siasa na uhusiano wa baadaye kati ya Tanzania na Jumuiya ya Ulaya.
Hata hivyo, mpaka sasa Roeland hajarudi nchini ambapo serikali haijaweza kutoa maelezo yoyote kuhusu ukimwa wa balozi huyo kurejea nchini.
Akiwasilisha taarifa ya upinzani Makamba amesema, serikali inapoona mabalozi wanakiuka mikataba ya Vienna, Bunge linapaswa kuelezwa kabla ya shinikizo.
“Kama serikali inaona kuna balozi zinakiuka mkataba wa Vienna katika utendaji wao, Bunge linapaswa kupewa taarifa kuwa ni mambo gani yanakiukwa,” amesema Salome.
Amesema, hakuna serikali yoyote inayoweza kufikia mipango yake bila kuwa na marafiki ama uhusiano na mataifa mengine duniani.
“Ni kwa bahati mbaya Tanzania inagombana na wahisani wanaowapatia misaada,” amesema Salome na kuhoji; “Kambi Rasmi ya Upinzani inapenda kujua ni kwa nini serikali imeanza kuziingilia balozi na kuziwekea mashinikizo kinyume na mkataba wa Vienna?”
Leave a comment