LENGAI Ole Sabaya, aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Hai, Mkoa wa Kilimanjaro na wenzake watano, wamesomewa mashtaka matano, katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha, ikiwemo unyang’anyi kwa kutumia silaha. Anaripoti Mwandishi Wetu, Arusha … (endelea).
Sabaya na wenzake watano, wamefikishwa katika mahakama hiyo leo Ijumaa, tarehe 4 Juni 2021, wakiwa katika gari ndogo ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru).
Sabaya na wenzake watano ambao ni; Sylivesta Nyegu, Wadson Stanley, Enock Togolan, John Odemba na Daniel Mbura, wamesomewa mashtaka matano katika kesi mbili tofauti mahakamani hapo.
Mashtaka mengine ni; uhujumu uchumi, unyang’anyi kwa kutumia silaha, kushiriki vitendo vya rushwa alipokea Sh.90 milioni, kutakatisha fedha na kuongoza magenge ya uhalifu.
Kesi ya kwanza, imesikilizwa na Hakimu Martha Mahumbuga na ya pili yenye ya jumla ya mashtaka mawili ya unyang’anyi kwa kutumia silaha na kushambulia aliowanyang’anya imesikilizwa na hakimu mwingine.
Nje ya Mahakama, mkurugenzi msaidizi ofisi ya mashtaka, anayeshughulikia usimamizi wa kesi, Tumain Kweka amesema, uchunguzi kwa baadhi ya makosa, “yanayomkabili Lengai na wenzake, yamefikia tamati ya kuwafikisha mahakamani.”
“Baada ya DPP kujiridhisha, ameamua kuwafikisha mahakamani, alikuwa anatuhumiwa kuendesha magenge ya uhalifu, vitendo vya rushwa, kutakatisha fedha na unyany’anyi wa kutumia silaha,” amesema Kweka.
Amesema, unyany’anyi wa kutumia silaha ni makossa mawili aliyoyatenda kwa watu wawili tofauti.
Mashtaka hayo kwa mujibu wa sheria, hayana dhamana hivyo, Sabaya na wenzake wamepelekwa gerezani hadi tarehe 18 Juni 2021, itakapotajwa tena.
Sabaya amefikishwa mahakamani baada ya kushikiliwa kwa zaidi ya siku kumi na Takukuru, kwa maagizo ya Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan.
Tarehe 13 Mei 2021, Rais Samia alimsimamisha kazi, Sabaya ili kupisha uchunguzi wa tuhuma mbalimbali zilizokuwa zinamkabili.
Hewallah – Safi sana.- Mbona hamtoi na habari za Manji? – Kama anashikiliwa na Takukuru ni lini atafikishwa mahakamani ili tujue makosa yake ni nini?