MWANASIASA mkongwe nchini Tanzania, Mzee Pius Msekwa, amesema muungano wa Tanganyika na Zanzibar, ulitokana na chimbuko la masuala matano, ikiwemo la kuimarisha ulinzi wa Visiwa hivyo baada ya mapinduzi matukufu yaliyotokea tarehe 12 Januari 1964. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Mzee Msekwa ametaja masuala hayo leo Jumanne, tarehe 26 Aprili 2022, akiwasilisha mada kuhusu chimbuko na misingi ya historia ya muungano wa Tanzania, kwenye maadhimisho ya sherehe za miaka 58 ya muungano huo, zilizofanyika jijini Dodoma.
“Chimbuko la muungano huu unaweza kuliweka katika maeneo matano tofauti, la kwanza mapinduzi matukufu ya Zanzibar yaliyofanyika tarehe 12 Januari. Bila mapinduzi hayo kusingekuwa na muungano,” amesema Mzee Msekwa.
Mwanasiasa huyo mkongwe nchini Tanzania, amesema sababu ya pili ilitokana na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, chini ya aliyekuwa Rais wa kwanza, Hayati Abeid Karume, kuhofiwa kupinduliwa, hivyo iliamua kujiunga na Tanganyika ili ipate msaada wa kijeshi.
“Chimbuko la pili kulinda usalama wa wananchi Zanzibar, kufuatia mapinduzi hayo kulikuwa na hofu huenda waarabu waliopinduliwa watajipanga upya kwa lengo la kurudi na kufanya mapinduzi kuiondoa Serikali,” amesema Mzee Msekwa.
Mzee Msekwa amesema “Zanzibar ilikuwa bado haiwezi kuunda jeshi lake dhidi ya uvamizi huo, kwa kushindwa huko ilikuwa dhahiri usalama wa Zanzibar ulikuwa hatarini, ukiwepo muungano haitakuwa na haja ya kuunda Jeshi lake kwani Jeshi la Tanganyika lilikuwa na uwezo wa kutosha kulinda Zanzibar.”
Sababu ya tatu iliyotajwa na Mzee Msekwa, ni utashi wa kisiasa kati ya Mwalimu Nyerere na Mzee Karume, huku la nne likiwa ni kuimarisha undugu kati ya wananchi huku ya mwisho ikiwa ni kiu ya uundwaji wa Umoja wa Afrika.
Leave a comment