MAMLAKA ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira jijini Mwanza (Mwauwasa) imesema, imepandisha bei ya maji kutokana na kuongezeka kwa gharama za uendeshaji. Anaripoti Moses Mseti, Mwanza … (endelea).
Sababu nyingine ni utengenezaji na ununuzi wa mitambo mipya ya uzalishaji wa maji, na kwamba mabadiliko ya bei hizo yameanza Julai Mosi mwaka huu.
Kauli hiyo imetolewa leo tarehe 6 Agosti 2019 na Meck Manyama, Kaimu Mkurugenzi wa Mwauwasa wakati akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake kuhusu sintofahamu iliyojitokeza kwa wananchi.
Manyama ambaye ni Ofisa Biashara Mwauwasa amesema, kabla ya kupandisha bei ya maji, walipeleka maombi na kupata kibali kutoka Wizara ya Maji na Umwagiliaji.
Amesema, wameamua kuongeza bei za maji kutoka Sh 14 kwa ndoo hadi shilingi 24 na senti 50 kwa wateja wakawaida (majumbani).
“Kimsingi uzalishaji wetu uliopo sasa hivi ni lita za ujazo 10,800 kwa siku, lakini uwezo huu katika chanzo chetu cha zamani umezidiwa, hivyo tukawaeleza uwezekano wa kujenga chanzo chetu kingine ambacho tayari tumeanza.
“Tumetangaza kujenga chanzo cha maji Butimba na maeneo mengine, na baada ya miradi hiyo kwa sasa tunachotakiwa kusimamia ubora wa huduma kwa wananchi. Tuliwaeleza bei hizi tunazopandisha, tunalenga kufanya ukarabati wa mabomba ya wateja wetu,” amesema Manyama.
Amesema, sababu nyingine ambazo waliwaeleza wadau wao ni pamoja na kujenga miradi mipya yenye kuongeza mitandao ya maji na kufikisha maji maeneo ambayo hayafiki.
“Wadau wote waliona umuhimu na kuridhia na kuiruhusu Mwauwasa kufanya mabadiliko ya maji, na kwa miaka minne mfululizo kiwango cha chini kabisa tulikuwa tunatoza Sh. 700 kwa uniti moja,” amesema Manyama.
Leave a comment