NAIBU Rais wa Serikali ya Kenya, William Ruto amesema kuwa kuna usaliti na vitisho vingi katika harakati za kuelekea Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika tarehe 9 Agosti mwaka huu. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Ruto ametoa kauli hiyo jana tarehe 2 Machi, 2022 wakati akizungumza katika mkutano uliodaliwa na taasisi Karson iliyopo chioni ya Chuo Kikuu cha Loyola – Maryland nchini Marekani.
Ruto kutoka Chama cha UDA yupo ziarani nchini Marekani akiwa ameambatana na swahiba wake, Musalia Mudavadi kutoka chama cha ANC.
Vyama hivyo viliungana rasmi mapema Disemba mwaka jana kuelekea katika uchaguzi mkuu wa taifa hilo la Afrika Mashariki.
Akizungumza katika mkutano huo Ruto alisema licha ya matumizi mabaya ya mfumo wa haki na kuwatisha viongozi ana imani atawania kiti cha urais.
“Wakenya watafanya uchaguzi huru. Tungetarajia kufanya hivi bila mizigo ya uhuni unaoendelea sasa lakini kwa bahati mbaya, ndipo tulipo,” alisema.
Hata hivyo, Ruto alisema kuwa watu wamesimama kidete kupinga hatua yoyote ya kufanya maamuzi kwa niaba yao.
“Kuna dhuluma nyingi, vitisho na matumizi ya mfumo wa haki ya jinai unaotumika kuwatisha viongozi pia kuwaomba watu kupiga kura kwa njia fulani. Nina imani kubwa kwamba matakwa ya watu wa Kenya yatashinda,” alisema.
Aidha, alibainisha kuwa masuala makubwa zaidi kwenye kura wakati wa uchaguzi mkuu wa Agosti ni kuzingatia demokrasia iwapo watu watapata fursa ya kufanya uchaguzi, bila ya udanganyifu na vitisho.
“Hilo ndilo linalohimiza msukumo wa sasa wa Wakenya wengi kusema hatupangwi, kumaanisha tunataka kufanya uchaguzi wetu bila kupangwa, kuongozwa au kutishwa,” alisema.
Maneno hayo ya Ruto yamekuja wakati kampeni zikiendelea nchini humo hususani katika kinyang’anyiro cha nafasi ya rais ambacho jicho kubwa linatupiwa kwa Kiongozi wa ODM, Raila Odinga na Ruto.
Licha ya Ruto kuwa Naibu Rais chini ya Rais wa sasa wa Kenya anayemaliza muda wake, Uhuru Kenyatta, wawili hao wametoafuatiana kisiasa kiasi cha Uhuru kutangaza hadharani kumuunga mkono aliyekuwa mpinzani wake kindakindaki Raila Odinga.
Leave a comment