MAHAKAMA ya Wilaya ya Babati, mkoani Manayara, imemhukumu kifungo cha miezi mitatu jela au kulipa faini ya Sh.600,000, Silvester Kayani, Afisa Uhamiaji wa Tanzania, kwa kukutwa na hatia ya kupokea rushwa ya Sh.100,000. Anaripoti Mwandishi Wetu, Manyara … (endelea).
Taarifa ya Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Mkoa wa Manyara, Holle Makungu aliyoitoa jana Jumanne, tarehe 16 Machi 2021, imesema, mtuhumiwa huyo ameshindwa kulipa faini na kupelekwa gerezani.
Amesema, Kayani alikuwa akituhumiwa kupokea rushwa ya shilingi laki moja, kutoka kwa mkazi mmoja wa Singida, ili asimchukulie hatua kutokna na tuhuma za uhamiaji haramu alizokuwa amezipokea dhidi ya raia huyo na mwisho wa uchunguzi, hakukuwa na ukweli dhidi ya raia huyo.
Makungu amesema, mtuhumiwa huyo, alifikishwa kwa mara ya kwanza mahakamani tarehe 26 Machim 2020 na kupatikana na hatia “na kuhukumiwa kifungo cha miezi mitatu jela au kulipa faini ya Sh.600,000.”
“Mshitakiwa alishindwa kulipa faini hiyo na hivyo kuanza kutumikia kifungo,” amesema Makungu kwenye taarifa yake kwa umma.
Amesema, kutokana na Kayani kukutwa na hatia ya makosa ya jinai mahakamani, “mtuhumiwa huyo anakuwa amepatikana pia na hatia kwa maana ya makosa ya kinidhamu na hivyo hatua za kumuondoa kwenye utumishi wa umma hufuatia.”
Leave a comment