JAMES Rugemalira, mfanyabiashara mkubwa na mshtakiwa wa kesi ya utakatishaji fedha, ameiomba Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam kufuatilia barua aliyoiandika kwenda kwa Kamishna wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA). Anaripoti Faki Sosi, Dar es Salaam…(endelea).
Hatua hiyo imekuja baada ya wakili wa serikali, Maghela Ndimbo kudai, upelelezi wa shauri hilo haujakamilika, wakati kesi hiyo ilipokuja kutajwa mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi leo tarehe 30 Januari 2020.
Rugemalira amedai kuwa, tarehe 24 Januari 24 2020, aliongea na mwakilishi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), alipotembelea gerezani na kumkabidhi nakala ya barua aliyoiandika kwenda kwa Kamishna wa TRA.
Amesema, kwenye barua hiyo amemeweleza Kamisha na TRA namna Benki ya Standard Chartered, Hongkong ilivyokuwa ikikwepa ushuru wa forodha.
Ameeleza, hajapata mrejesho wa barua hiyo, na kuomba kesi itakapotajwa tena mahakamani hapo, Takukuru ipeleke majibu kwasababu, wanaotakiwa kushitakiwa ni benki hiyo.
Rugemalira amedai, anashangaa kuona washtakiwa wengine wakiongezwa katika kesi hiyo na kusema kuwa, upelelezi hautokamilika kama watakua wanaongezwa. Na kwamba, ili upelelezi ukamilike, wafatilie nakala aliyowapelekea TRA.
Baada ya kusikiliza hoja hizo, Hakimu Shaidi amehairisha shauri hilo hadi tarehe 13 Februari 2020, ambapo itakuja kutajwa.
Harbinder Seth na Rugemalira kwa pamoja wanakabiliwa na mashitaka 12 yakiwemo ya utakatishaji fedha na kusababisha hasara ya Dola za Marekani 22,198,544.60 na Sh. 309,461,300,158.
Ni zaidi ya miaka miwili sasa, Seth na Rugemalira walipandishwa kizimbani kwa tuhuma hizo. Hata hivyo, inaelezwa ushahidi haujakamilika.
Leave a comment