MAHAKAMA ya Afrika Mashariki (EACJ) imetupilia mbali rufaa iliyokatwa na serikali, baada ya ushindi wa kesi ya kupinga baadhi ya vifungu vilivyoonekena kuwa kandamizi katika sheria ya huduma za vyombo vya habari ya mwaka 2016. Anaripoti Mwandishi Wetu, Arusha…(endelea).
Kesi hiyo iliyofunguliwa na Baraza la Habari Tanzania (MCT), Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC) na Kituo cha Sheri na Haki za Binadamu (LHRC).
MCT, THRDC na LHRC yaliiomba mahakama kufuta kusudio la Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kukata rufaa dhidi ya uamuzi wa mahakama hiyo, kupinga baadhi ya vifungu vya Sheria ya Huduma za Habari ya mwaka 2016, uliowapa ushindi MCT, THRDC na MCT mnamo tarehe 28 Machi 2019.
Januari mwaka 2017, kesi hii ilifunguliwa kwa pamoja na MCT, LHRC na THRDC katika hahakama hiyo wakitaka baadhi ya vifungu vifutwe kwa kuwa, vinakiuka mkataba unaoanzisha Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Baadaye tarehe 28 Machi 2019 Mahakama hiyo ilitoa hukumu iliyowapa ushindi MCT, THRDC na LHRC na kusema kuwa baadhi ya vifungu vya Sheria hiyo vinakiuka Mkataba unaoanzisha Jumuiya ya Afrika Mashariki na kuamuru vifutwe.
Kutokana na kutoridhika na uamuzi huo wa mahakama, upande serikali ulitoa taarifa ya nia ya kukata rufaa tarehe 11 Aprili 2019. Hata hivyo, haukuwahi kukata rufaa ndani ya siku 30 tangu tarehe ya kuonesha nia la kukata rufaa.
Kufuatia kuchelewa kukata rufaa, wanaoyawakilisha mashirika ya hayo waliwasilisha maombi ya kufuta kusudio la serikali ya kukata rufaa, mahakama hiyo imeamua kutupilia mbali rufaa hiyo.
Katika kesi hiyo, upande wa MCT, THRDC na LHRC uliwakilishwa na Mawakili Fulgence Massawe na Jebra Kambole wakati upande wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Tanzania uliwakilishwa na Mawakili Alicia Mbuya, Abubakari Mrisha na Stanley Kalokola.
Akizungumza baada ya uamuzi huo, Wakili wa LHRC, Fulgence Massawe amesema, ni jukumu la serikali kuanza kutekeleza ili sheria hiyo iendane na Mkataba wa Afrika Mashariki na kuachia uhuru wa kujieleza.
“Mahakama ya Afrika Mashariki uamuzi wake sio mapendekezo, ni uamuzi unofunga sehemu katika shauri hilo na kwa bahari nzuri, wametoa na gharama na wadau wataamua kama watadai hizo gharama ama la!,” amesema.
Leave a comment