MKUU wa Jeshi la Polisi Nchini (IGP), Simon Sirro amemteu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma (SACP), Lazaro Mambosasa kuwa Kamanda wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, anaandika Irene Emmanuel.
Kwa mujibu wa taarifa ya msemaji wa jeshi hilo, Barnabas Mwakalukwa, Sirro pia amemteua Kamishna Msaidizi wa Polisi (DCP), Juma Yusuf Ally kuwa Kaimu Kamishna wa Polisi Zanzibar.
Uteuzi wa makamanda hao unafuatia waliokuwapo kustaafu kwa mujibu wa sheria kwa kufikisha umri wa miaka 60.
Kabla ya uteuzi huo DCP Juma alikuwa ni Mkuu wa Utawala na Fedha Makao Makuu ya Polisi Zanzibar.
Sirro pia amewahamisha Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kipolisi Temeke Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP), Gilles Bilabaye Mroto kuwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma na Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Emmanuel Lukula kwenda kuwa Kamanda wa Polisi mkoa wa Kipolisi Temeke.
Leave a comment