ROKETI kadhaa zimerushwa kuelekea katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Kabul nchini Afghanistan, wakati ni siku ya mwisho kwa wanajeshi wa Marekani kuondoka nchini humo, Agosti 31 ikikaribia. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa … (endelea).
Ikulu ya Marekani imethibitisha mashambulizi hayo, ambayo inasema, hayajazuia operesheni inayoendelea kuwaondoa watu kutoka kwenye uwanja wa ndege.
Aidha, Afisa wa jeshi la Marekani amesema, baadhi ya roketi zilizuiwa na mitambo maalum, huku kundi la Islamic State likidai kutekeleza mashambulizi hayo.
Katika hatua nyingine, jeshi la Marekani linasema lilitekeleza shambulizi kwa kutumia ndege yake isiyokuwa na rubani hapo jana, kumlenga mlipuaji wa kujitoa mhanga aliyetaka kulipua uwanja wa ndege.
Raia 10 wa Afghanistan wakiwemo watoto sita waliouawa katika shambulizi hilo la Marekani, ambalo Washington inasema inachunguza kuhusu mauaji hayo.
Operesheni ya kuwahamisha raia wa Marekani na raia wa Afghanistan ambao maisha yao yapo hatarini, inatarajiwa kumalizika siku ya Jumanne tarehe 31 Agosti, 2021, siku ya mwisho kwa wanajeshi wa Marekani kuondoka nchini humo.
Leave a comment