MKUU wa Mkoa wa Rukwa, Joseph Mkirikiti ameeleza kutoridhishwa na matumizi ya zaidi ya Sh milioni 60 katika ujenzi wa Kituo kipya cha Afya cha Kasu wilayani Nkasi. Anaripoti Raheem Secha, Rukwa … (endelea).
Mkirikiti ametoa kauli hiyo leo tarehe 21 Oktoba, 2021 katika ziara ya aliyoanza mkoani humo kukagua miradi ya maendeleo.
Kutokana na hali hiyo amemuagiza Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, William Mwakalambile kusimamia ipasavyo matumizi ya fedha za serikali zilizoelekezwa mkoani humo kutekeleza miradi mbalimbali ikiwamo kituo hicho cha afya.
Akiwa kwenye eneo la mradi, Mkuu huyo wa mkoa alibaini matumizi yasiyo sahihi ya Sh milioni 60 zilizotumika kati ya Sh milioni 500 zilizotolewa na Serikali kujenga jengo la wagonjwa wa nje.
“Sijafurahishwa na mwenendo wa kazi ya ujenzi hapa. Inaonekana halmashauri hamjajipanga kukamilisha mradi huu unaosubiriwa mno na wananchi” amesema Mkirikiti
Amesema Serikali ilitoa Sh milioni 500 kwa halmashauri ya wilaya ya Nkasi kwa ajili ya ujenzi wa kituo kipya cha Afya Kata ya Kasu ambapo tayari kimeanza kujengwa kwa halamshauri kukusanya vifaa vya kazi.
Kwa upande wake Mkuu wa wikaya ya Nkasi, Peter Lijuakali amesema ataendelea kuhakikisha watendaji wa halmashauri wanazingatia matumizi sahihi ya fedha za umma na kuhakikisha miradi inakuwa bora.
“Nilifika hapa awali na kubaini matumizi ya Sh milioni 60 kinyume cha utaratibu kwani jengo hilo wanalodai ni OPD, liliianzishwa na wananchi tofauti na fedha zilizotolewa na serikali Sh milioni 500 za sasa hivyo nikaaagiza lisimame,” alisema Lijuakali.
Mkirikiti ameanza ziara ya siku mbili kwenye wilaya ya Nkasi kukagua miradi ya elimu, afya, bandari ya Kabwe. Pia anatarajiwa kuzungumza na wananchi kutoa elimu namna ya kujikinga na maambukizi ya UVIKO-19 kwa kujitokeza kupata chanjo.
Leave a comment