WAKUU wa mikoa ya Pwani na Morogoro wamesema wamejipanga kuhakikisha umeme utakaozalishwa kupitia Mradi wa Bwawa la Julius Nyerere (JNHPP), unachochea shughuli za maendeleo na kijamii kwa wananchi wao. Anaripoti Selemani Msuya, Rufiji, Pwani … (endelea).
Pia viongozi hao wameahidi kuulinda na kuutunza mradi utakaozalisha megawati 2,115, ambao unagharimu zaidi ya Sh.trilioni 6.5 ili uweze kuwa endelevu.
Akizungumza wakati wa zoezi la kujaza maji kwenye bwawa hilo lililofanywa na Rais Samia Suluhu Hassan leo katika eneo la mradi wilayani Rufiji, Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Abubakar Kunenga amesema ukamilifu wa mradi huo unaenda kichocheo shughuli za uzalishaji mkoani kwake.
Kunenga amesema mradi huo utawezesha umeme katika mkoa huo kupatikana kwa asilimia 100 hivyo kuongeza uzalishaji.
“Mheshimiwa Rais sisi Pwani tunashukuru bwawa hili la JNHPP kuwepo hapa Rufiji, tunaamini Watanzania watanufaika ila Pwani itanufaika zaidi, nikiahidi kwa kushirikiana na wenzetu wa Morogoro tutaulinda na kuutunza,”amesema.
Aidha, Kunenga amemuomba Rais kuangalia uwezekano wa kukamilisha ujenzi wa barabara kutoka Mwanarumango hadi kwenye mradi kwa kiwango cha lami, ili kurahisisha kufika eneo husika.
Mkuu huyo wa mkoa amesema barabara kutoka Kisarawe hadi JNHPP ni fupi na rahisi kufikika hivyo anamuomba Rais Samia kutenga bajeti ya ujenzi.
Naye Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Fatma Mwasa alisema ameomba ujenzi wa bwawa hilo uwe ni neema na kwa wananchi wa mkoa huo kwa kupatiwa huduma za afya, elimu na nyinginezo.
“Sisi tunaomba mradi huu ukianza tupate mgao kupitia CSR ili tuweze kujenga Hospitali ya Rufaa ya kisasa, chuo cha afya na mengine,” amesema.
Mwasa ameungana na Kunenga katika kuhakikisha miradi huo inalindwa na kutunzwa.
Leave a comment