ALIYEWAHI kuwa mkuu wa mikoa ya Dodoma, Mara, Mtwara na Arusha kwa nyakati tofauti, Isdory Shirima amefariki dunia leo tarehe 31 Machi 2023. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa Itikadi na Uenezi, Sophia Mjema, CCM kimepokea kwa masikitiko na huzuni taarifa ya kifo cha mkuu huyo wa mkoa mstaafu.
Mjema pia amemtaja Shirima kuwa kwa nyakati tofauti aliwahi kushika dhamana mbalimbali ndani ya CCM, ikiwa ni pamoja na Katibu Msaidizi Mkuu (CCM) – Idara ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa, Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) na Katibu wa Chama Cha Mapinduzi Mkoa wa Tanga.
Amesema CCM kitamkumbuka Shirima alivyokuwa mwanachama, mtumishi na Kiongozi mwaminifu, aliyetumia uwezo wake kwa maslahi mapana ya CCM na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na nchi kwa ujumla.
“CCM chini ya Uongozi wa Mwenyekiti wa Chama, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan, kinatoa salaam za pole kwa familia ya marehemu, ndugu, jamaa, marafiki na wanachama wa CCM na wote walioguswa na msiba huu. Mungu ailaze roho ya marehemu mąhali pema peponi, Amina,” amesema mjema katika taarifa hiyo.
Leave a comment