MKUU wa mkoa wa Tanga, Omary Mgumba, amelezea faida za uwepo wa chuo cha mafunzo cha uhamiaji mkoani Tanga ikiwemo kuimarisha ulinzi na usalama wa nchi kwani eneo hilo hutumika sana kama mapito ya wahamiaji haramu. Anaripoti Urumasalu Kusung’uda, TUDARCo…(endelea).
Mgumba ameyasema hayo leo Jumatatu tarehe 15 Agosti 2022, katika hafla ya uwekaji jiwe la msingi wa chuo hicho uliofanywa na Rais Samia Suluhu Hassan sambamba na kufunga mafunzo ya awali ya askari wa uhamiaji kozi namba 1/2022.
Amesema eneo hilo lilikuwa likitumika kwa biashara haramu ya binadamu kwa uhamiaji haramu kwani ndiko walikokuwa yakipita majahazi kwenda sehemu mbalimbali “hivyo basi uwepo wa chuo hiki kitazuia uhamiaji haramu.”
Pia amesema ujenzi wa chuo hicho umeleta maendeleo katika mkoa wa Tanga ikiwemo kuboreshwa kwa miundombinu mbalimbali kama ujenzi wa zahanati itakayotoa huduma kwa wananchi wa mkoa huo hususani wakazi wa wilaya ya Mkinga pia uanzishwaji wa mradi mkubwa wa maji unaogharimu zaidi ya bilion 40, “haya yote ni manufaa kwa wananchi wa wilaya hii.”
Mgumba ameongezea kuwa jeshi hilo ni jipya hivyo litatoa ajira kwa wananchi ambapo kwa sasa jumla ya askari 818 wamehitimu mafunzo ya jeshi hilo.
“Watu wanapata mafunzo sio kwa maaskari wa hamiaji peke yake bali na maaskari wengine na kubadilishana mafunzo na jinsi ya kukabiliana na uhalifu kwani ni jeshi kamili na sio taasisi,” amesema.
Leave a comment