MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam (RC) nchini Tanzania, Amos Makalla, amesema majeruhi wa tukio la mauaji lililotokea jirani na Ubalozi wa Ufaransa nchini humo, wanaendelea vizuri. Anaripoti Mwanaharusi Abdallah, TUDARCo … (endelea).
Makalla ametoa taarifa hiyo leo Ijumaa, tarehe 27 Agosti 2021 katika shughuli ya kuiaga miili ya Askari Polisi watatu na mlinzi mmoja wa Kampuni ya Ulinzi ya SGA, iliyofanyika viwanja vya Polisi, Kurasini mkoani Dar es Salaam.
Amesema jana Alhamisi alitembelea Hospitali ya Taifa ya Muhimbili na Hospitali ya Polisi Kilwa Road Kurasini, na kuzungumza na majeruhi hao.
“Jana mimi na wenzangu tulikuja hospitali mochwari tuliwaona wote pamoja na mhalifu, vijana wadogo ambao walikuwa tegemeo kwa nchi yetu.”
“Hatukuishia hapo, tulikwenda kuwaona majeruhi wote mmoja wa hapa na mwingine Muhimbili, niseme watapona tumewaona wameeleza kwa kina tukio lilivyotokea itoshe kusema tumepoteza mashujaa,” amesema Makalla.
Pia, mkuu huyo wa mkoa ametoa rambirambi ya Sh.6 milioni na kumpatia Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Simon Sirro atakayezigawa kwa familia za marehemu wote wanne.
Leave a comment