HALMASHAURI ya jiji la Mbeya imeagizwa ndani ya miezi mitatu iwe imekamilisha ujenzi wa mnara wenye hadhi na uandikwe majina yote ya mashujaa kutoka Mkoa wa Mbeya ambao walifariki dunia wakati wa vita ya pili ya dunia kati ya mwaka 1939-1945 kama kumbukumbu nzuri kwa kizazi kijacho. Anaripoti Kenneth Ngelesi, Mbeya … (endelea)
Agizo hilo limetokewa leo Jumatatu, tarehe 25, Julai, 2022, na Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Juma Homera wakati wa maadhimisho ya Siku ya Mashujaa iliyofanyika kwenye eneo walipozikwa mashujaa hao ambapo maofisa mbalimbali wa Serikali pamoja waliweka mashada kwenye makaburi hayo.
Homera amesema haridhishwi na namna yalivyo andikwa majina hayo kwa sasa kwani hayalingani na kazi waliyofanya mashujaa hao.
Amesema mara baada kujenga mnara yataandikwa upya majina ya mashujaa wote ambao walishiriki ambapo hivi sasa majina yao yameandikwa kibao ambacho hakionekani.
“Meya na Mkurugenzi wa Jiji mpo, natoa miezi mitatu mjenge mnara mkubwa hapa na majina ya mashujaa wetu yaandikwe, hatuwezi kuwa tunaadhimisha siku ya mashujaa halafu majina ya mashujaa yamejificha ili kulinda heshima ya mashujaa wetu,” amesema Homera.
Amesema katika eneo hilo kuna kibao kidogo ambacho kimeandikwa majina ya mashujaa hao lakini hakiweki kumbukumbu sahihi na hivyo ili kuwaenzi vizuri ni lazima ujengwe mnara mkubwa.
Katika hatua nyingine Homera amewapongeza viongozi hao wa Jiji la Mbeya kwa kulisimamia vizuri eneo hilo na kulifanyia usafi mara kwa mara na kuwa safi wakati wote na kuelendelea kuwa na mvuto.
Naye katibu Tawala Mkoa wa Mbeya, Dk. Angelina Lutambi amesema mashujaa hao waliozikwa katika eneo hilo walifariki wakati wakilipigania Taifa lao jambo ambalo linatakiwa kuendelea kufundishwa kwa vijana.
Amesema vijana wa Tanzania wanatakiwa wajifunze kupigania taifa lao kama ambavyo mashujaa hao walipoteza maisha wakiwa kwenye mapambano dhidi ya wakoloni na vita ya Kagera mwaka 1978.
Amesema mashujaa hao waliofariki walionesha uzalendo kwa Taifa lao kutokana na kufariki wakati wanapigania haki mbalimbali za taifa lao na kwamba ni muhimu kuwawekea kumbukumbu sahihi.
Leave a comment