MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam (RC) nchini Tanzania, Amos Makalla ameongeza muda wa siku 12 kwa wanaofanya biashara maeneo yaliyokatazwa kuhama na kuwataka kutumia muda huo kuhamia kwenye maeneo yaliyotengwa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Ameyataja maeneo wanayopaswa kuondoka ni wanaofanya biashara maeneo ya watembea kwa miguu, hifadhi ya barabara, mbele ya maduka, maeneo ya umma na waliojenga vibanda juu ya mitaro na mifereji.
RC Makalla aliongeza muda huo jana Jumatatu, tarehe 18 Oktoba 2021, alipokwenda kuzungumza na wafanyabiashara wa Kariakoo. Ilikuwa ni siku ya mwisho waliokuwa wamepewa kuhamia maeneo yaliyotengwa.
Alisema, ameamua kuongeza muda huo ili kutoa fursa ya kutosha wa machinga hao kuhama na ukimalizika asionekane mfanyabiashara yoyote kwenye maeneo yaliyokatazwa.
Mkuu huyo wa mkoa alitoa maelekezo kwamba, eneo la DDC liboreshwe ili liweze kupokea wafanyabiashara wengi zaidi tofauti na sasa ambapo linatumika kuuza vyakula na vinywaji.
Aidha, Makalla amefurahishwa na mwitikio mzuri wa wafanyabiashara kuhamia kwenye maeneo yaliyotengwa na kutoa wito kwa wengine kutumia muda uliotolewa kuhama.
Miongoni mwa sababu zinazofanya Serikali kuamua kuwapanga vizuri Machinga ni kupotea kwa mandhari ya Jiji Kutokana na uchafu, ongezeko la ajali na foleni.
Pia, sababu za kiusalama kutokana na vibanda vilivyojengwa kutumika kuhifadhi wahalifu nyakati za usiku na upotevu wa mapato ya serikali kutokana na wafanyabiashara wakubwa kuwatumia machinga kukwepa kodi.
Leave a comment