RAIS wa Afrika Kusini, Cyril Ramaphosa amesema tatizo la umeme limeathiri kwa kiwango kikubwa sekta ya madini ambayo ni nguzo muhimu ya uchumi. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa … (endelea).
Ramaphosa ametoa kauli hiyo leo tarehe 8 Februari 2023 alipokuwa akihutubia katika mkutano mkubwa wa Afrika wa uwekezaji katika madini wa Indaba.
Baraza la Madini la Afrika Kusini, ambalo linawakilisha makampuni ya uchimbaji madini, linakadiria kuwa jumla ya ujazo wa madini ulipungua kwa asilimia sita sawa na Dola za Marekani bilioni 1.8 mwaka jana.
Katika hotuba yake, Rais Cyril Ramaphosa alikiri kwamba ukatikaji wa umeme uliotokea kwa siku 200 mwaka 2022, kuchangia kushuka kwa madini.
“Tatizo la umeme limeleta athari kubwa katika sekta ya madini kama ilivyokuwa kwa sekta nyingine. Miezi sita iliyopita, tulitangaza mpango wa kitaifa wa utekelezaji wa nishati ili kuboresha utendaji kazi wa vituo vyetu vya umeme vilivyopo na kuongeza uwezo wa uzalishaji mpya kwenye gridi ya taifa haraka iwezekanavyo,” amesema.
Ramaphosa amesema serikali sasa inaruhusu makampuni ya madini kuzalisha umeme wao wenyewe bila vikwazo vyovyote hali ambayo italeta mabadiliko makubwa.
Mchumi mkuu wa baraza la madini la Afrika Kusini, Henk Langenhoven, amesema hotuba ya rais iligusa vidokezo vyote vinavyofaa kuhusu ni hatua gani inachukuliwa kutatua matatizo.
“Nadhani ukweli kwamba mgao unamgusa kila mwananchi na kila mpiga kura ni muhimu kushughulikia jambo hilo. Na hivi majuzi tumeona uharaka na msukumo kutoka kwa rais, na hazina yetu ya kitaifa ina oparesheni ya pamoja hasa kwa kuangalia hili. Na wamekuwa wakifanya kazi sana kujaribu na kuharakisha ili hatua zitekelezwe haraka iwezekanavyo,” amesema.
Mkutano wa uwekezaji wa madini wa Afrika, Indaba, unaofanyika katika kituo cha kimataifa cha mikutano cha Cape Town unamalizika kesho Alhamisi.
Leave a comment