RAIS wa Zambia, Hakainde Hichilema amefanya mabadiliko ya uongozi katika vyombo vya ulinzi na usalama, siku sita baada ya kuingia madarakani, tarehe 24 Agosti 2021. Anaripoti Patricia Kighono, TUDARCo … (endelea).
Rais Hichilema ametangaza mabadiliko hayo jana Jumapili, tarehe 29 Agosti 2021, kupitia ukurasa wake wa Twitter.
“Leo jioni tumefanya mabadiliko katika vyombo vya ulinzi na usalama vya Taifa letu,” imesema taarifa ya Rais Hichilema.
Kupitia taarifa hiyo, Rais Hichilema amesema Luteni Jenerali Dennis Alibuzwi, ameteuliwa kuwa Kamanda wa Jeshi la Zambia, huku msaidizi wake akiwa ni Meja Jenerali, Geoffrey Zyeele.
Luteni Jenerali Collins Barry, ameteuliwa kuwa Kamanda wa Jeshi la Anga la Zambia (ZAF), huku naibu wake akiwa ni Meja Jenerali Oscar Nyoni.
Luteni Jenerali Patrick Solochi, ameteuliwa kuwa Kamanda wa Huduma ya Kitaifa ya Zambia (ZNS), msaidizi wake akiwa Meja Jenerali Reuben Mwewa.
Pia, Rais Hichilema amemteua Remmy Kajoba, kuwa Inspekta Jenerali wa Polisi nchini humo, huku naibu wake katika masuala ya operesheni, akiwa ni Milner Myambango, wakati Doris Chibombe, akiwa naibu upande wa utawala.
Mabadiliko hayo yamefanyika tangu Rais Hichilema aapishwe kuwa kiongozi wa Zambia, baada ya kumshinda aliyekuwa Rais wa Taifa hilo, Edgar Lungu, katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika tarehe 12 Agosti 2021.
Hichilema aliyekuwa mgombea wa Chama Kikuu cha Upinzani Zambia, United Party for National Development (UPND), alishinda kiti cha urais baada ya kupata kura milioni 2.8 wakati Lungu aliyegombea kwa chama cha Patriotic Party, akishika nafasi ya pili akipata kura milioni 2.8.
Leave a comment