RAIS wa Zanzibar, Ali Mohamed Shein amewateua Khamis Ramadhan Abdalla na Aziza Iddi Suweid kuwa majaji wa Mahakama Kuu ya Zanzibar, anaandika Hamis Mguta.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka kwenye tovuti ya Ikulu ya Zanzibar uteuzi huo umeanza jana na umefanyika kwa mamlaka aliyopewa chini ya kifungu cha 94(2) cha Katiba ya Zanzibar ya 1984.
Aidha, kwa mujibu wa uwezo wake chini ya Sheria ya Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma Namba 4 ya 2015, kama ilivyorekebishwa na Sheria Namba 4 ya 2017, Kifungu cha 10(a)(1), amemteua, Kubingwa Mashaka Simba kuwa Katibu wa Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma.
Katika uteuzi mwingine, Shein chini ya kifungu cha 6(2) cha Sheria ya Shirika la Bandari Namba 1 ya 1997, amemteua Kapteni Juma Haji Juma kuwa Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Bandari.
Rais Shein pia amemteua George Joseph Kazi kuwa Naibu Katibu Mkuu katika Ofisi ya Rais, Katiba, Sheria, Utumishi wa Umma na Utawala Bora anayeshughulikia masuala ya Katiba na Sheria.
Viongozi wa hao walioteuliwa wanatarajiwa kuapishwa Ikulu ya Zanzibar Oktoba 2, mwaka huu .
Leave a comment