RAIS Samia Suluhu Hassan, amesema mwanzoni Wizara ya Maji ilikuwa inampa tabu katika utekelezaji wa majukumu yake, lakini kwa sasa inakwenda vizuri kwa kuhakikisha miradi yake inatekelezwa kikamilifu. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea).
Mkuu huyo wa nchi ya Tanzania, ametoa kauli hiyo leo Jumatatu, tarehe 6 Juni 2022, Ikulu jijini Dodoma, akishuhudia utiaji saini mikataba ya miradi ya maji ya miji 28.
“Ni ukweli wizara ya maji mmebadilika sanasana, mlinipa tabu mwanzo tulielezana ukweli mambo ya kubuni miradi mikubwa kuliko inayotakiwa. Mko kwenye mstari tunakwenda vizuri. Mradi huu badala ya miji 16, tunakwenda mpaka 28,” amesema Rais Samia.
Rais Samia amesema, siku za nyuma wizara hiyo ilikabiliwa na changamoto ya kubuni miradi mikubwa kuliko kiwango kinachotakiwa, sambamba na kushindwa kubana matumizi, lakini kwa sasa changamoto hizo zimepungua.
“Kuna eneo yalihitaji mabomba sita tu lakini kwenye ubunifu kuna 21. Vile mmerudi mmekaa vizuri mradi unakwenda kunufaisha wengi. Hata miradi inayotekelezwa sasa mmejitahidi kubana matumizi. Pahali pa mradi mmoja, unazaa fedha za kuanzia mradi mwingine. Ahsanteni naomba muendelee hivyo,” amesema Rais Samia.
Akitaja mafanikio ya wizara hiyo, Rais Samia amesema chini ya Waziri wake, Jumaa Aweso, imefanikiwa kuokoa miradi ya maji 126, iliyokwama kwa sababu mbalimbali.
Leave a comment