RAIS Samia Suluhu Hassan amewataka wanawake wote Tanzania kuweka mipango vizuri ili katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025 wamuweka rais mwanamke madarakani kwa sababu nafasi aliyonayo sasa ni kwa kudra za Mwenyezi Mungu. Anaripoti Patricia Kighono, TUDARCo … (endelea).
Pia amesema iwapo wanawake wataikosa nafasi hiyo ya urais Mungu atawalaani.
Rais Samia ametoa kauli hiyo leo tarehe 15 Septemba 2021 wakati akihutibia katika maadhimisho ya siku ya demokrasia duniani yaliyofanyika kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee, jijini Dar es salaam.
Amesema licha ya kwamba amepewa tuzo na majukwaa mbalimbali ya wanawake waliohudhuria maadhimisho hayo, bado wanawake hawajamuweka rais madarakani.
“Niwaambie wanawake bado hatujaweka rais mwanamke madarakani, amekaa kwa sababu ya kudra za Mwenyezi Mungu na matakwa ya Kikatiba.
“Tulichochangia sisi na dada zetu na mama zetu ni ile kusukuma mpaka mwanamke amekuwa makamu wa rais, lakini kufika hapa kama sio kudra ya Mungu ingekuwa Mungu sana. Rais mwanamke tutamuweka mwaka 2025,” amesema.
Amesema ifikapo mwaka 2025 kisha wanawake wakashikamana na kumuweka rais mwanamke, watakutana tena kwenye kongamano kama hilo kwa furaha.
“Wameanza kutuchokoza kwa kuandika kwenye kigazeti Samia hatawania urais nani kawaambia?
“Fadhila za Mungu zikija mikononi mwako usiziachie, hizi ni fadhila za Mungu, wanawake wamefanya kazi kubwa kuleta uhuru wa nchi hii katika kujenga siasa, tumebeba wanaume katika siasa za nchi, leo Mungu ametupatia baraka, tukiiachia Mungu atatulaani,” amesema Rais Samia.
Leave a comment