RAIS wa Tanzania Samia Suluhu Hassan, amesema Serikali yake inataka kuurejesha Mkoa wa Kigoma katika hadhi ya kitovu cha biashara kwa kufungua fursa za kibiashara kati ya mkoa huo na nchi jirani. Anaripoti Mwandishi Wetu, Kigoma … (endelea).
Rais Samia ametoa ahadi hiyo leo Jumanne, tarehe 18 Oktoba 2022, akizungumza na wananchi wa mkoa huo, akiweka jiwe la msingi la upanuzi wa Bandari ndogo ya Kibirizi, mkoani Kigoma.
Amesema, Serikali yake imeamua kuijenga bandari hiyo kisasa ili biashara kati ya Tanzania na nchi jirani zinazopakana na Kigoma, zifanyike kwa ufanisi mkubwa.
“Tunafanya hivyo kwa sababu tunataka kuirejesha Kigoma kuwa kitovu cha biashara, ndiyo maana mambo meni tunaleta sasa hivi Kigoma. Tunajenga bandari, umeme wa kutosha tunaleta ili watu waweze kufanya biashara vizuri, wawekezaji waje na mambo mengine,” amesema Rais Samia.
Aidha, Rais Samia amemuagiza Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa, kuusadia Wakala wa Barabara za Vijijini na Mjini (TARURA),kujenga barabara inayoingia bandarini hapo.
Huku akiuagiza uongozi wa Mkoa wa Kigoma kwa kushirikiana na uongozi wa wafanyabiashara wadogo, kujenga upya vibanda vya biashara vilivyo karibu na eneo la bandari.
“Nakwenda kutafuta fedha za kujenga eneo hilo naomba nanyi muanze kujipanga, mjipange kupitia umoja wenu wa wafanyabiashara, tukubaliane jinsi patakavyotengenezwa hapo ili mtu akitoka bandarini pazuri akute na wafanyabiashara wamekaa pazuri na biashara inaendelea,” amesema Rais Samia.
Leave a comment