TANZANIA imeahidi kuingia kwa miguu miwili katika uwekezaji nchini Kenya. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Kauli hiyo imetolewa na Rais Samia Suluhu Hassan akimwambia Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya leo Jumanne, tarehe 4 Mei 2021, katika viwanja vya Ikulu nchini humo.
“Kenya imewekeza Tanzania miradi 513 yenye thamani ya Dola za Marekani 1.7 bilioni na kutoa ajira zipatazo 51,000 kwa Watanzania.
“Zipo kampuni 30 za Watanzania zilizowekeza mtaji ndani ya Kenya wenye thamani ya shilingi za Kenya Bi.19.3 na kutoa ajira kwa watu 2640, lakini nikaweka ahadi kwamba, Tanzania tutakuja kwa miguu yote kuwekeza Kenya,” amesema Rais Samia.
Amesema, Kenya ndio mwekezaji wa kwanza katika Jumuiya ya Afrika Mashariki katika uwekezaji Tanzania, na kwamba kwa ujumla duniani inashika namba tano kuwekeza Tanzania.
Rais huyo amesema, Tanzania na Kenya ni wadau wakubwa wa biashara ambapo katika miaka mitano iliyopita, wamefanya biashara ya wastani wa Tsh. 1 trilioni na kwamba, sio kubwa.
Rais Samia amesema, wamekubaliana na Rais Kenyatta
kuendelea kushughulikia changamoto ikiwa ni pamoja na vikwazo vya kodi.
Kwenye mazungumzo yake, ameshauri tume ya ushirikiano iwe inakaa na kupitia changamoto baina ya nchihizo mbili kisha kutoa suluhu.
Amesema, mawaziri wa afya wa Tanzania na Kenya, wakae na kuangalia namna ya kurahisisha mfumo wa kuangalia na kuchunguza virusi vya corona (COVID-19), watu wapate huduma za haraka.
“Tumejadiliana kuhusu namna ya kutekeleza miradi ya kimkakati, na mradi wa bomba la gesi tumesaini leo ambapo kinachofuata ni utekelezaji.
“Tumejadilia kuhusu kuimarisha jumuiya yetu Afrika Mashariki (EAC) na pamoja na kuhimizana kulipa michango yate,” amesema.
Rais Samia amemwalika na kumtaka Rais Kenyatta kuwa mgeni rasmi katika sherehe za maadhimisho ya siku ya Uhuru wa Tanzania tarehe 9 Desemba 2021.
“Mwaka huu 9 Desemba, Tanzania tunatimiza miaka 60 ya Uhuru, nimemuomba Rais Kenyatta awe mgeni rasmi,” amesema.
Leave a comment